Barabara ya Dar es Salaam - Arusha yafungwa kwa muda baada ya daraja kujaa maji

Muktasari:

Kutokana na daraja la mto Mnyuzi liliopo katika kijiji cha Mandera Wilaya ya Handeni  kujaa maji, polisi kitengo cha usalama barabara mkoa wa Tanga, kimefunga kwa muda barabara hiyo kwa muda na sasa magari yote yanapitia Handeni mjini.

Handeni. Barabara kuu ya kutoka Dar es salaam kwenda mikoa ya Kaskazini Arusha, Kilimanjaro, Manyara na nchi jirani ya Kenya imefungwa kwa muda na Jeshi la Polisi kitengo cha Usalama  Barabarani kutokana na daraja kujaa maji katika kijiji cha Mandera mpakani mwa Wilaya ya Handeni na Korogwe mkoani Tanga, Tanzania.

Akizungumza na Mwananchi leo Jumapili asubuhi Oktoba 13,2019, Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoani Tanga, Solomon Mwangamilo amesema tangu jana saa tisa jioni, hali haikuwa shwari.

Amesema maji mengi ya mvua yalikuwa yakipita juu ya daraja hilo na kusababisha  njia kufunga hadi sasa.

 “Nikiwa sambamba na timu yangu tulifunga njia ya Mkata na kuelekeza magari yote yaendayo Korogwe na mikoa ya kaskazini kupitia Handeni, katika daraja lile (mto Mnyuzi)  hali ni mbaya haturuhusu magari kupita, magari yote kutoka Arusha, Kilimanjaro na maeneo mengine yapitie Handeni mjini, hadi hali itakapotengamaa,” amesema Kamanda Mwangamilo. 

Amesema barabara ya kutoka Tanga kwenda Dar es Salaam hali siyo mbaya.

Kamanda huyo amesema ni eneo moja tu lililopo Muheza ndilo madereva wanapaswa kuchukua tahadhari, lakini maeneo mengine  hayana tatizo.

Ametoa wito kwa madereva wawe waangalifu, waache kudharau taarifa wanazopewa na askari wake ili kujinusuru kwenye maeneo hatarishi huku akiwataka pia kuendesha mwendo mdogo  kwa sababu barabara zinateleza.

Akizungumzia adha hiyo, msafiri Digna Tesha amesema hali katika eneo hilo ni tete, maji bado mengi na hajui watanasuka saa ngapi.

Kadhalika, imeelezwa kuwa magari yanayotoka Turiani mkoani Morogoro kwenda Handeni yameshindwa kuendelea na safari baada ya daraja la barabara ya kijiji cha Kang'ata kufunikwa na maji.