Bashungwa ataka washiriki kampuni 100 bora tangu mwaka 2011 kukutanishwa

Muktasari:

Waziri wa Viwanda na Biashara nchini Tanzania, Innocent Bashungwa ameshauri kuandaliwa mkutano utakaozikutanisha kampuni zote zilizoshiriki mchakato wa kutafuta kampuni 100 bora tangu kuanza kwa mashindano hayo mwaka 2011.

Dar es Salaam. Waziri wa Viwanda na Biashara nchini Tanzania, Innocent Bashungwa ameshauri kuandaliwa mkutano utakaozikutanisha kampuni zote zilizoshiriki mchakato wa kutafuta kampuni 100 bora tangu kuanza kwa mashindano hayo mwaka 2011.

Amesema Serikali itashirikiana na kampuni ya Mwananchi Communication’s Ltd (MCL) na kampuni ya Hesabu ya KPMG kuandaa mkutano huo ili kujua kampuni hizo zipo wapi na zinafanya nini.

Bashungwa ametoa kauli hiyo leo Alhamisi Oktoba  24, 2019 katika mkutano wa mchakato wa kutafuta kampuni 100 bora ambao kilele chake kitakuwa kesho Ijumaa Oktoba 25, 2019.

"Kaka Francis (Nanai-Mkurugenzi Mtendaji wa MCL) ataanza kuhofia gharama, sapoti itakuwepo naomba mtengeneze kanzi data ya kampuni zote zilizowahi kushiriki," amesema Bashungwa.

Amesema mkutano huo utasaidia kujua kampuni hizo zilikotoka, zilipo na zinakoelekea ili kuona namna ya kuzisaidia.

"Mkutano huo uwe fursa ya kuona namna ya kuzisaidia kampuni ndogo na za kati,” amesema Bashungwa.

Kwa upande wake Nanai amesema, “tumechukua tutaandaa huo mkutano, asante sana kutushika mkono tutakutafuta muda ukifika."