Benki ya CBA, GSM wazindua ofa maalumu

Mkurugenzi Mtendaji wa Benkiya CBA Tanzania, Dk. Gift Shoko (kushoto) na Meneja Mkuu wa Mauzo na Masoko – GSM, Allan Chonjo (kulia) wakibadilishana mkataba wa makubaliano kati ya kampuni hizo mbili unaokusudia kuwapa wateja wa CBA fursa ya kutumia huduma za kidigitali.Picha na Michael Matemanga

Dar es Salaam.  Kuna mambo ukiyasikia au kuyashuhudia unajua wazi kuwa mwaka umeelekea ukingoni, sherehe za mwisho wa mwaka nazo zipo karibu.

Hivi sasa zimebakia siku zisizozidi 72 kumaliza mwaka na mara nyingi wakati huu ni kawaida kushuhudia punguzo la bei la bidhaa na huduma mbalimbali, wafanyabiashara hufanya hivyo ili kuvutia wateja katika kipindi hicho ambacho watu wengi wanakuwa mapumzikoni.

Leo Oktoba 21, 2019, Benki ya CBA Tanzania kwa kushirikiana na maduka ya GSM wamezindua ofa maalumu kwa ajili ya msimu wa sikukuu na baadaye.

 Kwa mujibu wa ofa hiyo, wateja wa CBA watakaofanya manunuzi ya samani katika maduka hayo na kulipa kwa kadi watapata punguzo la asilimia 15 ya bei.

 Akizungumza wakati wa utiaji saini wa makubaliano kati ya kampuni hizo mbili, Mkurugenzi Mtendaji wa CBA Tanzania, Dk Gift Shoko amesema ushirika huo unatarajia kuwaongeza idadi ya wateja wa benki hiyo wanaotumia kadi katika malipo.

Ushirikiano huo unakusudia kuwapa wateja wote wa sasa na wapya wa benki hiyo fursa ya kutumia huduma za kidijitali.

Mkuu wa masoko na mauzo wa maduka ya GSM, Allan Chonjo amesema kampuni hiyo imeingia makubaliano na Benki ya CBA ili kupanua wigo wa kibiashara.

“Tunaamini kuwa ubora wa bidhaa zetu ni mkubwa na kulingana na mwitikio wa watu tunaweza kuongeza na bidhaa za aina nyingine katika ofa hii,” amesema.