VIDEO: DC azikutanisha familia za bilionea Msuya, aomba maridhiano

Muktasari:

  • Mkuu wa Wilaya Arumeru mkoani Arusha, Jerry Muro amezikutanisha familia za Bilionea Erasto Msuya ili kupata maridhiano kutoka pande zote na kusisihi kukubali kumaliza mvutano ulipo wa mali za ndugu yao aliyefariki mwaka 2013 kwa kupigwa risasi.

Arusha. Kikao cha kugombea mali za Bilionea Erasto Msuya ambaye aliuawa  mwaka 2013 kinaendelea ofisi ya Mkuu wa Wilaya Arumeru mkoani Arusha, Jerry Muro ambaye anazitaka familia zote kukubali maridhiano.

Akizungumza katika kikao hicho leo Jumatatu Oktoba 21, 2019, Muro anasema ni muhimu familia ya Msuya na familia ya Miriam Mrita ambaye ni alikuwa mke wa Bilionea Msuya kukubali kwamba kila familia imeathirika na mauaji ya Msuya.

"Hapa hatutafuti  mshindi mama na baba wa Msuya tayari mlimpoteza mtoto Erasto lakini na wewe mtoto Kelvin umempoteza baba yako na mama yako yupo Gegerezani, sasa mali za Msuya zisiwafanye mpate laana" amesema.

Awali, Wakili Shilinde Ngalula anayewatetea watoto wa Bilionea Msuya anasema wakati muafaka huo unatafutwa pia izingatiwe hata Mjane wa Msuya, Miriam yupo gerezani katika kesi inayohusu mali.

Wakili Shilinde amesema kuna mambo mawili yanaweza kufanywa kumaliza mgogoro, kuna kesi tatu zilifunguliwa kumpinga mjane wa marehemu kusimamia  mirathi zinaweza kufutwa.

"Aliyepeleka anaweza kwenda kufuta, katika kesi ya mjane, shihidi namba moja ni Mama wa Erasto Ndeshukuru Sikawa sasa tutapata vipi muafaka wakati kuna kesi mahakamani," amesema.

Hata hivyo, Mkuu huyo wa  wilaya ametaka wakati wa kusaka suluhu suala la mke wa Bilionea Msuya litakuja baada ya maridhiano ya familia.

"Hakuna ambaye anasema mjane wa Msuya sio msimamizi wa mirathi hivyo, tuache kesi ya jinai inayomkabili mke wa Msuya," anasema

Kelvin Msuya anaomba maridhiano kupatikana na ambao wanataka kuchukua mali za baba yake waache.

Dada wa Msuya, Ester Msuya aliomba serikali kusaidia kugawanywa mali za Msuya kwa haki na wote wenye haki wapate wakiwepo watoto.

Kikao bado kinaendelea.

Endelea kufuatilia Mwananchi kujua kinachoendelea