De Gea atema nyongo Man United

Muktasari:

  • David de Gea amesema mwenendo wa Manchester United ni mbaya na haukubaliki kwa namna yoyote.

London, England. Kipa David de Gea amesema kiwango cha Manchester United msimu huu kinasikitisha.

De Gea alisema hakuwahi kuona Man United mbovu tangu alipojiunga na klabu hiyo kama ya msimu huu.

Kipa huyo ametoa kauli hiyo muda mfupi baada ya Man United kulala bao 1-0 dhidi ya Newcastle United jana, kwenye Uwanja wa St James Park.

Dea Gea alisema anapitia kipindi kigumu katika maisha yake ya soka na ametaka hatua zichukuliwe kuinusuru klabu hiyo.

“Hatukutengeneza nafasi za kufunga. Tunatakiwa kuongeza kasi. Sina la kusema, ndio tuna majeruhi lakini hakuna msamaha,”alisema kipa huyo wa kimataifa wa Hispania.

De Gea alidai Man United inaweza kubadilika na kucheza kwa kiwango bora kama kutakuwa na mkakati wa pamoja.

“Tuko vitani bado tuna nafasi ya kubadilika kila mmoja akapambana kwa nguvu zake zote, sisi ni wamoja tunaweza,”alidokeza De Gea.

Bao la Midfielder Matty Longstaff limeendeleza machungu kwa kocha wa Man United Ole Gunnar Solskjaer.

Solskjaer atakuwa kikaangoni katika mchezo ujao dhidi ya watani wao wa jadi Liverpool kwenye Uwanja wa Anfield Oktoba 20.

Man United imeshindwa kurejea katika kiwango katika ubora tangu alipostaafu aliyekuwa Kocha Sir Alex Ferguson mwaka 2012.