Diamond kutua Moshi, kupanda Mlima Kilimanjaro

Muktasari:

Msanii Diamond ni kati ya wasanii watakaopanda Mlima Kilimanjaro kesho Jumamosi Septemba 27, 2019 katika kampeni ya 'Kili Challenge Twenzetu Kileleni.'

 


Moshi. Msanii wa Bongofleva nchini Tanzania, Diamond Platnumz ni kati ya wasanii watakaoungana na kikundi cha watu 130 kupanda mlima Kilimanjaro kesho.

Upandaji huo wa mlima Kilimanjaro ulioshirikisha wasanii wa Bongofleva, filamu, waandishi wa habari ni sehemu ya kampeni ya kuhamasisha Utalii wa ndani iliyopewa jina la "Kili Challenge Twenzetu Kileleni.

Akizungumza na Mwananchi, Waziri wa Maliasili na Utalii nchini Tanzania, Hamis Kigwangala amesema Diamond anatarajia kufika Moshi leo Ijumaa Septemba 27, 2019 ambapo ataongozana na wasanii wengine akiwemo MwanaFa na Madee.

Kuhusu ushirikishwaji wa wasanii amesema wizara imeamua kuwatumia kwa kuwa ni watu wenye kuhamasisha vitu vingi kwenye jamii. 

"Huwezi kuhamasisha watu kupanda Mlima Kilimanjaro kwa kuandika tu kwenye ukurasa wako bali fanya kwa vitendo wakuone na wewe umeenda inapendeza zaidi na kufanya peke yangu kama waziri siwezi bila kuwahamasisha wadau wengine wakiwemo wasanii," amesema Waziri Kigwangalla.

Katika hatua nyingine,  Waziri Kigwangalla aliambatana na wapanda mlima hao kutembelea maporomoko ya Kilasia na kuhimiza watu kwenda kuweza kujionea uzuri wake.