Guardiola: Raheem? Hakuna kama Ronaldo na Messi duniani

Muktasari:

Kocha wa Manchester City amesema angependa winga wake Raheem kufikia viwango vya Ronaldo na Messi, lakini amesema bado hajafikia na hakuna mchezaji yeyote duniani anayeweza kulinganishwa na wawili hao.

 


Manchester, Uingereza (AFP).Pep Guardiola angepanda Raheem Sterling kufikia kiwango sawa na Lionel Messi na Cristiano Ronaldo, lakini kocha huyo wa Manchester City hana uhakika kuna mchezaji atakayeweza kufikia kiwango cha nyota hao wawili duniani.

Baadhi ya watu wamekuwa wakimlinganisha Sterling na nyota hao wawili waliotaweala soka la takriban miaka kumi iliyopita.

Kocha wa England, Gareth Southgate alisema Sterling atafikia wakati ambao atakuwa akitajwa sambamba na Messi na Ronaldo alipoulizwa kiwango gani cha mafanikio winga huyo wa England anaweza kufikia kama akiendelea na mafanikio yake ya sasa.

Beki wa zamani wa Liverpool, Jamie Carragher pia amesema kuwa anamuona Sterling kuwa na uwezo wa kushinda tuzo ya Mwanasoka Bora wa Dunia, tuzo ambayo imekuwa ikitwaliwa na nyota wa Barcelona, Messi na mshambuliaji wa Juventus, Ronaldo; kila mmoja akitwaa mara tano.

Kocha wa City, Guardiola amefurahishwa na maendeleo ya Sterling katika miaka mitatu aliyofanya naye kazi, lakini akiwa pia amemfundisha Messi katika klabu ya Barca, anajua viwango visivyo vya kawaida vinavyotakiwa kufikia kilele hicho.

"Kwa sasa, Raheem hajafikia kiwango hicho, lakini labda baadaye ningependa iwez hivyo. Kwetu itakuwa ni kutimia kwa ndoto kwake na wengine," Guardiola aliwaambia waandishi.

"Kuiwa katika kiwango kilekile kwa watu hawa wawili, ni magwiji, wana kitu kisicho cha kawaida katika ulimwengu wa soka.

"kama Raheem anaweza kupania kufikia kiwango hicho –- wow. Tutakuwepo kumsaidia na bila shaka anaweza.

"Lakini kwa sasa, hakuna mtu, si kwenye klabu hii, au kwenye klabu zote anayeweza kulinganishwa na wawili hawa na kile walichokifanya kila wiki kwa miaka kumi, Hakuna."

Sterling alikuwa na msimu mzuri mwaka jana, akifunga mabao 25 na kuiwezesha City kutwaa vikombe vitatu vya England; Ligi Kuu, Kombe la FA na Koimbe la Ligi.