Lampard atoa ya moyoni Chelsea

Muktasari:

Kocha wa Chelsea, Frank Lampard amewataka wachezaji wake kuongeza kasi katika mechi za mashindano ya Ligi Kuu England, baada ya jana kulazimishwa sare ya bao 1-1 dhidi ya Leicester City


London, England. Frank Lampard amesema wachezaji wake wanahitaji ukomavu ili kukabiliana na mikikimikiki ya Ligi Kuu England.

Kocha huyo ametoa kauli hiyo, baada ya Chelsea kulazimishwa sare ya bao 1-1 dhidi ya Leicester City.

Chelsea jana ilitangulia kupata bao lililofungwa na Mason Mount kabla ya Wilfred Ndidi, kusawazisha.

Lampard amewataka wachezaji wake kuongeza kasi ili kuipa mafainikio Chelsea katika mechi za mashindano.

“Tumeonyesha kiwango, tulishindwa kulinda ushindi wetu, mpira una nidhamu. Ni jambo jema kila mchezaji ameonyesha kitu,” alisema Lampard.

Kiungo huyo wa zamani wa England, alisema anatarajia mechi ijayo itakuwa ya mafanikio.

“Kimsingi mtazamo wangu wa leo (jana) ni kushinda mechi, nimejifunza kitu baada ya matokeo haya. Nawashukuru mashabiki kutuunga mkono na nipo hapa kikazi,” alisema Lampard.

Nguli huyo amewaondoa hofu mashabiki wa Chelsea baada ya kuanza vibaya kibarua chake akijaza nafasi ya Maurizio Sarri aliyejiunga na Juventus.

Mechi ya kwanza ya Ligi Kuu England Chelsea ilifungwa mabao 4-0 dhidi ya Manchester United kabla ya kuchapwa 5-4 kwa penalti ilipovaana na Liverpool katika mechi ya fainali ya Uefa Super Cup.