Maalim Seif asema Dk Bashiru hawezi kubadili siasa za Zanzibar

Muktasari:

Mshauri mkuu wa Chama cha ACT- Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad amesema katibu mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally hawezi kuibadili siasa ya Zanzibar.

Unguja. Mshauri mkuu wa Chama cha ACT- Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad amesema katibu mkuu wa CCM, Dk Bashiru Ally hawezi kuibadili siasa ya Zanzibar.

Maalim Seif amesema Dk Bashiru hata akipewa miaka tisa hawezi kubadili siasa za kisiwani humo alizodai kuwa ni tofauti na za Tanzania Bara.

Ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Desemba 6, 2019 wakati akikusanya maoni ya wanachama wa chama hicho kwa ajili ya kutengeneza ilani ya uchaguzi ya ACT-Wazalendo mwaka 2020.

Amesema  siasa ya Zanzibar ni tofauti na maeneo mengine mengi ya Tanzania na Afrika, “watu wengi upinzani wao upo moyoni si rahisi kubadili misimamo yao.

Amefanya ziara ya siku tisa mimi nataka nimpe miaka tisa hataweza kuibadili siasa ya Zanzibar hususani kisiwani Pemba.”

Maalim Seif amesema ni ngumu kwa kuwa wananchi walio wengi wanakosa  haki zao za msingi ikiwemo kazi kwa kile alichokiita ubaguzi katika sekta ya ajira.