VIDEO: Mabasi mwendokasi yaoshwa mara mbili

Dar es Salaam. Ili kukabiliana na mlipuko wa ugonjwa wa virusi vya corona kwenye vyombo vya usafiri, uongozi wa mabasi yaendayo haraka (BRT) umesema hivi sasa yanaoshwa mara mbili kwa siku.

Machi 19, Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri Ardhini (Latra) ilitoa maelekezo mbalimbali kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kujikinga na maambukizi ya corona.

Miongoni mwa maelekezo hayo, wamiliki wanatakiwa kunyunyuzia dawa za kuua virusi katika mabasi yao huku mabasi ya BRT yakitakiwa kubebea idadi ya abiria iliyoanishwa kwenye leseni.

Mkurugenzi wa kampuni ya mabasi yaendayo haraka (Udart), John Nguya aliliambia Mwananchi jana kuwa sasa mabasi hayo yanaoshwa mara mbili kwa siku tofauti na awali ili kuongeza juhudi za kupambana na virusi hivyo kwenye usafiri.

Nguya alisema katika mchakato wa kuyaosha watumia dawa kali yenye nguvu ya kuua vijidudu mbalimbali, shughuli hiyo inatekelezwa na kampuni ya Suma JKT.

“Shughuli hii inafanyika katika ghala letu Jangwani nyakati za asubuhi na mchana. Tumeamua kuongeza nguvu ili kuunga juhudi za Serikali kukabiliana na ugonjwa wa virusi hivi,” alisema.

Mbali na hilo, Nguya alisema hivi sasa abiria wanaingia katika mabasi kwa mfumo wa foleni kuepuesha watu kujazana, lakini mchakato umekuwa ukikumbwa na changamoto mara kwa mara kwani watu hawapo tayari kuufuata.

“Tuomba ushirikiano wa abiria ukiambiwa basi limejaa basi subiri siyo kulazimisha kupanda,” alisema.

Alitoa mfano wa basi linalotakiwa kuchukua watu 90, hivi sasa kwa mazingira yalivyo linapaswa kubeba 80.