Madaktari kuteta na Rais John Magufuli Februari 20

Muktasari:

Madaktari wajipanga kumuelezea Rais Magufuli changamoto zao katika mkutano utakaofanyika Februari 20, mwaka huu

Dar es Salaam. Rais John Magufuli anatarajiwa kukutana na watumishi wa sekta ya afya ikiwa ni kuelekea maadhimisho ya siku ya madaktari inayotarajiwa kufanyika Machi 4.

Mkutano huo utakaofanyika Februari 20, 2020  Jijini Dar es Salaam, utahusisha  madaktari na watumishi wa sekta ya afya zaidi ya 1,000 kutoka katika maeneo mbali.

Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania (MAT) Dk Elisha Osati amesema mkutano huo muhimu unalenga kumkutanisha Rais Magufuli na watumishi hao ili kuzungumzia changamoto na mafanikio ya sekta hiyo.

Dk Osati amesema miongoni mwa mambo watakayomueleza Rais ni changamoto zinazowakabili ikiwemo suala la ajira kwa madaktari na watoa huduma katika sekta hiyo.

Changamoto nyingine ni motisha kwa watoa huduma pamoja na wanasiasa kuwaingia madaktari wakiwa katika utekelezaji wa majukumu yao.

“Tunaona taarifa za wizara zinasema kuna upungufu wa watoa huduma lakini kuna madaktari wengi wako mitaani hawana ajira.”

“Katika kipindi hiki ambacho serikali inafanya maendeleo makubwa katika sekta ni muhimu kuangalia uendelevu wa huduma zinazotolewa” amesema Dk Osati.