Magufuli ataja sababu sherehe za Uhuru kufanyika Mwanza

Muktasari:

Rais wa Tanzania, John Magufuli amesema maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanganyika yamefanyika mjini Mwanza kuondokana na kufanya mambo kwa mazoea.

Mwanza. Rais wa Tanzania, John Magufuli amesema maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanganyika yamefanyika mjini Mwanza kuondokana na kufanya mambo kwa mazoea.

Kiongozi mkuu huyo wa nchi ametoa kauli hiyo leo Jumatatu Desemba 9, 2019  wakati akizungumza katika maadhimisho hayo yanayofanyika katika uwanja wa CCM Kirumba.

"Ikumbukwe kuwa hatukufanya sherehe hizi kwa miaka miwili, mwaka 2015 na mwaka 2018  badala yake fedha zake zilifanya kazi za maendeleo.”

"Hivyo hivyo ndio sababu  tukaamua tufanye sherehe hizi mkoani Mwanza  tofauti na ilivyozoeleka, hii ni kwa sababu ya kubadili mazoea,” amesema Magufuli.

Amesema sherehe hizo huambatana na fursa mbalimbali, kuchochea maendeleo ya Mkoa huo.

Magufuli amesema miongoni mwa mambo ya kujivunia tangu nchi ipate uhuru ni kulinda amani, upendo na kudumisha muungano.

Amesema zipo nchi nyingi zilizopata uhuru miaka mingi lakini hazina amani kuwataka  wananchi kuendelea kuilinda amani hiyo.