Magufuli kukipandisha hadhi kituo cha afya Mwanga

Mgombea urais wa CCM, John Magufuli

Muktasari:

Mgombea urais wa CCM, John Magufuli yupo kwenye mikutano ya kampeni ambapo ameahidi kutatua changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi wilayani Mwanga.

 

Mwanga.Mgombea urais wa CCM, John Magufuli ameahidi kukipandisha hadhi kituo cha afya Mwanga na kuifanya kuwa hospitali ya wilaya.

Pia Magufuli ameahidi kujenga kituo cha mabasi  katika wilaya ya Mwanga pamoja na kujenga soko la samaki ili kudhibiti uvuvi haramu.

Magufuli amesema hayo, leo Oktoba 22 kwenye mkutano wa kampeni uliofanyika viwanja vya Cleopa  David Msuya wilayani Mwanga na kueleza hakuna ubaya wilaya ikiwa na hospitali mbili.

 "Mwanga kuna hospitali ya wilaya ambayo ipo Usangi ni mlimani, lakini kwa heshima ya Mzee Msuya, Joseph Tadayo na wananchi nitajenga hospitali nyingine ya wilaya hapa Mwanga Mjini na hakuna ubaya kukiwa na hospitali mbili za wilaya," amesema.

Amesema hawezi kukosa fedha na kushindwa kupandisha hadhi kituo cha afya Mwanga na kuifanya kuwa hospitali ya wilaya.

"Natambua pia mnahitaji stendi ya mabasi, niachieni hili. Atakapochaguliwa mbunge na madiwani wa CCM, nitasaidia kuona uhakika wa kupata kituo cha mabasi hapa Mwanga mjini."