Mahakama yataifisha Sh16.7 bilioni kuwa mali ya Serikali ya Tanzania

Muktasari:

Mahakama Kuu kitengo cha ufisadi imetaifisha Sh16.7 bilioni na kuwa mali ya Serikali leo Ijumaa Aprili 3, 2020.

Dar es Salaam. Mahakama Kuu kitengo cha ufisadi imetaifisha Sh16.7 bilioni na kuwa mali ya Serikali leo Ijumaa Aprili 3, 2020.

Fedha hizo zilikuwa za washtakiwa watatu waliokuwa wakiendesha biashara ya upatu, kutakatisha fedha na kula njama katika kesi ya uhujumu uchumi iliyokuwa inawakabili.

Washtakiwa hao ni raia wa Ujerumani, Manon Huebenthal; Frank Rickets ambaye ni raia  Uingereza na kampuni ya IMS Marketing Tanzania Ltd.

Uamuzi huo umetolewa  na Jaji Elinaza Luvanda wa mahakama hiyo  baada ya mkurugenzi wa mashtaka Tanzania, Biswalo Mganga kuwasilisha maombi mahakamani hapo akitaka kiasi hicho cha fedha kitaifishwe na kuwa mali ya Serikali.

Mganga alichukua uamuzi huo kwa sababu tangu washtakiwa hao wafunguliwe kesi katika mahakama ya hakimu mkazi Kisutu hawajawahi kutokea  mahakamani.