Mahakama yatupa ombi la DC Chemba kutaliki, yamtaka kutoa Sh250,000 kila mwezi za mtoto

Mkuu wa Wilaya ya Chemba, Simon Odunga akiwa katika Mahakama ya Ukonga jijini Dar es Salaam leo. Kushoto ni Mke wake wa nje  ya ndoa Ratifa Vicent . Picha na Anthony Siame

Muktasari:

Mahakama ya Mwanzo ya Ukonga, Dar es Salaam nchini Tanzania imekataa ombi la Mkuu wa Wilaya ya Chemba (DC) mkoani Dodoma, Simon Odunga kumtaliki Ruth Osoro

Dar es Salaam. Mahakama ya Mwanzo ya Ukonga, Dar es Salaam nchini Tanzania imekataa ombi la Mkuu wa Wilaya ya Chemba (DC) mkoani Dodoma, Simon Odunga kumtaliki Ruth Osoro.

Hakimu Elia Mrema ametoa hukumu hiyo leo Ijumaa Agosti 23,2019  baada ya kusikiliza ushahidi uliotolewa na mashahidi wa pande zote.

Mbali na kukataa ombi la talaka, imemuamuru Odunga kutoa Sh250,000 za matunzo ya mtoto kila mwezi, kuanza sasa hadi atakapofikisha umri wa miaka 18. Mtoto huyo hivi sasa ana umri wa miaka minne. Odunga pia ametakiwa kugharamia matibabu na masomo ya mwanaye.

Akitoa hukumu hiyo, hakimu Mrema amesema Mahakama  ilijiuliza endapo kuna ndoa halali baina ya Odunga na Ruth.

Alifafanua tafsiri ya ndoa ni muungano wa hiari kati ya mume na mke kwa kusudi la kuishi pamoja katika siku zote za maisha yao.

Amebainisha katika sheria ya ndoa, kuna ndoa ya mke mmoja na ndoa ya mke zaidi ya mmoja.

Hakimu Mrema amesema kulingana na cheti cha ndoa iliyofungwa bomani kati ya Odunga na Ruth inaonyesha mkuu huyo wa wilaya hajawahi kuoa wala mdaiwa hajawahi kuolewa.

Lakini kabla ya kuhitimisha cheti hicho cha ndoa, Mahakama ilikilinganisha na ushahidi uliotolewa mahakamani hapo na Odunga ambao haukuwa na uwazi kuwa wakati anamuoa Ruth mwaka 2010, mwanamke huyo alikuwa akitambua kuwa  anaishi na mwanamke mwingine na akaridhia.

Kwa  habari zaidi soma gazeti la Mwananchi kesho Jumamosi Agosti 24,2019