Majaliwa atoa maagizo kwa Ma RC

Muktasari:

  1. Waziri mkuu wa Tanzania Kassim Majaliwa awataka wakuu wa mikoa kusimamia halmashauri zao ili ziweze kujenga miradi mikubwa ya kimkakati kwa kutumia mapato ya ndani badala ya kutumia mapato hayo kwa posho na safari


Geia. Waziri Mkuu nchini Tanzania, Kassim Majaliwa amewataka wakuu wa mikoa kote nchini kuzisimamia halmashauri zao ili zijenge miradi mikubwa ya kimkakati kwa mapato ya ndani badala ya kuzitumia kwa kulipana posho na safari.

Akizungumza leo Jumapili Septemba 22, 2019 wakati wa ufunguzi wa maonyesho ya pili ya teknolojia ya dhahabu katika viwanja vya Kalangalala mjini Geita, Majaliwa amesema halmashauri zinakusanya fedha nyingi  za kutosha lakini hakuna miradi mikubwa inayotekelezwa kwa makusanyo ya ndani.

"Halmashauri zetu zinakusanya fedha nyingi za kutosha wengine bilioni mbili wengine bilioni tatu lakini hakuna mradi hata mmoja mkubwa hata wa milioni 200 unaoonyesha ni makusanyo ya ndani ipo midogomidogo fedha nyingi utasikia posho na safari" amesema Majaliwa

Aidha amezitaka halmashauri kubadilika na kuwataka wakuu wa mikoa kusimamia halmashauri zao kuhakikisha miradi mikubwa inajengwa

Badala ya kusubiri fedha kutoka Serikali Kuu.

Waziri mkuu amezitaka halmashauri kujenga miradi ya kimkakati ikiwemo vituo vya mabasi, soko na barabara badala ya kusubiri Serikali Kuu kuja kujenga kilometa moja wakati halmashauri ina uwezo wa kujenga kilomita 15 kwa wakati mmoja.