Majaliwa awasimamisha wajumbe bodi ya mkonge

Muktasari:

  • Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewasimamisha wajumbe wa bodi ya wakurugenzi ya mkonge Tanzania (TSB) na kumteua katibu wa tume ya kufuatilia  mali za bodi hiyo, Saddy Kambona kuwa mkurugenzi wa bodi hadi itakapotangazwa vinginevyo.

Tanga. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa amewasimamisha wajumbe wa bodi ya wakurugenzi ya mkonge Tanzania (TSB) na kumteua katibu wa tume ya kufuatilia  mali za bodi hiyo, Saddy Kambona kuwa mkurugenzi wa bodi hadi itakapotangazwa vinginevyo.

Ametoa agizo hilo leo Ijumaa Machi 6, 2020 katika kikao cha watumishi wa bodi ya mkonge na viongozi wa Serikali ambacho ajenda ilikuwa  kupokea taarifa zaidi ya uchunguzi uliofanywa na tume hiyo kuhusu mali za bodi hiyo zilizokuwa zimehujumiwa.

Wajumbe wa bodi ya wakurugenzi waliosimamishwa ni Mark Njiu, Fredie Semwaiko, Lady Swai, Deogratius Ruhinda, Abdallah Ngereza, Betty Machangu , Dk Nyambilila Amur na Revelian Ngaiza.

Amesema wote isipokuwa mwenyekiti wa bodi hiyo, Mariam Nkumbi watakaa pembeni ili kuipa nafasi tume kuendelea na uchunguzi wa mali zinazodaiwa kuhujumiwa hadi zitakaporejeshwa serikalini.

Majaliwa amemuelekeza Kambona kufanya kazi za kila siku zilizokuwa zikifanywa na aliyekuwa mkurugenzi wa bodi hiyo, Yunnus Msika pamoja kusimamia mwenendo mzima wa bodi kwa kushirikiana na Nkumbi.

Majukumu mengine ya viongozi hao walioteuliwa na Majaliwa ni  kuwa na mamlaka ya kuchukua  hatua stahiki kwa  yeyote aliyehusika na ubadhilifu wa mali za bodi.

“Mali za iliyokuwa mamlaka ya mkonge watu waligawana kijanja

huku bodi ya mkonge ikiwa ipo na hakuna bodi nyingine iliyoshiriki

kuuza kinyume cha sheria. Serikali inataka kuona mali zote zinarudishwa na kila aliyehusika kuhujumu atachukuliwa hatua,” amesema Majaliwa.

Awali, Kambona alimweleza Majaliwa kuwa zimechukuliwa hatua za kurejesha serikalini mali za bodi hiyo zilizokuwa zimezuiwa, kugawiwa kienyeji yakiwemo majengo na vitega uchumi.