Majaliwa kufanya ziara ya siku mbili Kigoma

Muktasari:

Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa anatarajiwa kufanya ziara ya siku mbili mkoani Kigoma

Kigoma. Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa anatarajiwa kufanya ziara ya siku mbili mkoani Kigoma.

Akizungumza leo Ijumaa Julai 12, 2019 mkuu wa Mkoa wa Kigoma, Emmanuel Maganga amesema  Majaliwa atawasili mkoani humo kesho Jumamosi Julai 13, 2019.

Akiwa Kigoma atatembelea shughuli za maendeleo na utekelezaji wa ilani ya uchaguzi ya CCM mwaka 2015.

Pia, ataongoza kongamano la Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) la kumpongeza na kumuombea Rais wa Tanzania,  John Magufuli.

Maganga amesema waziri mkuu atatembelea kituo cha Kihinga cha utafiti wa zao la mchikichi na baadaye kukutana na viongozi wa CCM na Serikali.

Aidha Mkuu wa mkoa huyo amewaomba wakazi wa Kigoma na mikoa ya jirani kujitokeza kwa wingi kupokea waziri Mkuu wa Tanzania.