VIDEO: Makamu wa Rais Mama Samia aongoza maadhimisho miaka 43 ya kuzaliwa CCM

Makamu wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan

Muktasari:

Maelfu ya wanachama wa CCM kutoka katika wilaya zote tano za Dar es Salaam wakiambatana na viongozi wao wamehudhuria maadhimisho hayo huku wakiwa wamevaa mavazi ya rangi za chama hicho ambazo ni kijani na njano.

Dar es Salaam. Maelfu ya wanachama wa CCM wa Mkoa wa Dar es Salaam wamehudhuria sherehe za maadhimisho ya miaka 43 ya kuzaliwa kwa chama chao.

Sherehe hizo zinafanyika leo Februari 13, 2020 jijini hapa na Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni mlezi wa CCM Mkoa wa Dar es Salaam akiwa ndiyo mgeni rasmi katika maadhimisho hayo.

Maelfu ya wanachama wa CCM kutoka katika wilaya zote tano za Dar es Salaam wakiambatana na viongozi wao wamehudhuria maadhimisho hayo huku wakiwa wamevaa mavazi ya rangi za chama hicho ambazo ni kijani na njano.

Viongozi wengine waliohudhuria maadhimisho hayo ni pamoja na mwenyekiti wa CCM mkoa wa Dar es Salaam, Kate Kamba, mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda pamoja na wakuu wote wa wilaya za Dar es Salaam.

Wengine ni wabunge wa CCM mkoa wa Dar es Salaam, Mwita Waitara (Ukonga), Mussa Azan Zungu (Ilala) na Angela Kairuki (viti maalumu) pamoja na Kaimu meya wa Jiji la Dar es Salaam.

CCM ilianzishwa Februari 5, 1977 na mwaka huu imetimiza miaka 43. Maadhimisho hayo katika mkoa wa Dar es Salaam yamefanyika leo ikiwa ni mwendelezo wa maadhimisho yanayofanyika katika mikoa mbalimbali nchini.