Makonda aeleza sababu kuchelewa mkutano wa viongozi wa dini

Muktasari:

Mwenyekiti wa Kamati ya Amani Mkoa wa Dar es Salaam, Shekh Alhad Mussa Salum amesema Makonda amepona kukumbwa na upepo wa kisulisuli baada ya kuwasili katika kongamano maalum la viongozi wa dini.

Dar es Salaam. Saa kadhaa baada  ya Mwenyekiti wa kamati ya Amani ya Mkoa wa Dar es Salaam, Sheikh Alhad Mussa kuonyeshwa kusikitishwa kwake na kitendo cha viongozi wa mkoa huo kutohudhuria kongamano la viongozi wa dini leo Jumatatu Oktoba 28,2019, hatimaye Mkuu wa mkoa huo,  Paul Makonda aliwasili mkutanoni hapo.

Makonda aliwasili kwenye ukumbi wa mkutano Saa 6:30 mchana wakati kongamano hilo lilianza Sa 3:35 asubuhi katika ukumbi wa JNICC likihuisha viongozi wa dini mbalimbali.

Awali, Mwenyekiti wa Kamati ya Amani Mkoa wa Dar es Salaam, Shekh Alhad Mussa Salum alieleza kusikitishwa na hatua ya viongozi wa mkoa huo kutofika kwenye kongamano hilo.

Wakati Makonda akiwasili, Shekh Salum alisema, “Mheshimiwa Mkonda asubuhi nilikusema, umepona na upepo wa kisulisuli.”

Punde baada ya kuwasili Makonda alieleza sababu za kuchelewa kwake na akieleza kuwa ni majukumu ya kiofisi.

 “Nilikuwa nakimbia  ubungo kwenda kuangalia eneo la ujenzi wa hospitali ya wilaya, tumepata fedha juzi kwa hiyo tunataka Jumatano ujenzi uanze,” amesema Makonda na kuongeza;

“Tunakosa usingizi, mambo mengi yamebadilika kwa sababu watu wengi sio waaminifu na hawana hofu ya Mungu. Watu hawatimizi majukumu yao.”