VIDEO: Makonda amwomba Majaliwa kutoa neno mikopo ya wasanii

Muktasari:

Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa ni mgeni rasmi katika kongamano la Sanaa la Mwalimu Nyerere jijini Dar es Salaam ambapo Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda amwomba Majaliwa kushughulikia suala la mikopo kwa wasanii.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam nchini Tanzania, Paul Makonda amemuomba Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Kassim Majaliwa kutoa neno kuhusu kusuasua kwa mikopo ya wasanii.

Makonda amesema hayo leo Ijumaa Novemba 15, 2019 jijini Dar es Salaam nchini Tanzania wakati wa kongamano la Sanaa la Mwalimu Nyerere ambalo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa ndiye mgeni rasmi akimwakilisha Rais wa Tanzania, John Magufuli.

Akizungumza katika kongamano hilo, Makonda amesema mkoa huo uliomba ridhaa ya Bunge kwamba wasanii wapewe mikopo isiyo na riba kupitia fedha za manispaa lengo ni kuwawezesha kuendesha shughuli zao.

“Mwaka jana tulipata nafasi ya kwenda Dodoma bungeni katika uwasilishaji wa bajeti. Tuliomba wasanii wakopeshwe mikopo isiyo na riba, wabunge walituelewa na wakatupa nafasi  hiyo.”

“Jambo hili linasuasua na halijafikiwa katika malengo, wasanii wanaambiwa waandike maandiko wanajitahidi wanaandika kila aina ya maandiko lakini hawapewi hizo fedha,” amesema

Makonda amesema fedha hizo zingekuwa zinatolewa ingepunguza malalamiko ya wasanii kukandamizwa na wasambazaji wa kazi zao.