Makonda atembelea machinjio Vingunguti usiku

Muktasari:

  • Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Tanzania, Paul Makonda usiku wa kuamkia leo Jumatatu Oktoba 14, 2019 ametembelea machinjio  ya Vingunguti na kuwahamasisha wafanyabiashara kujiandikisha kushiriki uchaguzi wa Serikali za mitaa.

Dar es Salaam. Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Tanzania, Paul Makonda usiku wa kuamkia leo Jumatatu Oktoba 14, 2019 ametembelea machinjio  ya Vingunguti na kuwahamasisha wafanyabiashara kujiandikisha kushiriki uchaguzi wa Serikali za mitaa.

Makonda aliyeagiza leo maduka kufunguliwa saa 5 asubuhi ili kumuenzi mwalimu Julius Nyerere ambaye leo ni kumbukumbu ya miaka 20 ya kifo chake, amewataka wananchi kujiandikisha ili kupata fursa ya kushiriki uchaguzi huo.

Katika mitandao mbalimbali ya kijamii kuna video zikimuonyesha Makonda akizungumza na wafanyabiashara wa Vingunguti pamoja na kukagua ujenzi wa machinjio ya kisasa.

Makonda amewahimiza wafanyabiashara hao kujiandikisha kuchagua viongozi watakaomsaidia Rais wa Tanzania, John Magufuli.

“Kuna kero mtaani sasa ni uamuzi wako kujiandikisha ili umpate mwenyekiti wa mtaa atakayeungana na rais kukamilisha safu itakayopinga rushwa, isiyokuwa na ujanja ujanja na itakayoleta maendeleo,” amesema Makonda.