Malengo matano ukuaji wa uchumi 2019/2020 yaanikwa

Mbunge wa Nyamagana, Stanslaus Mabula akisoma kitabu cha hotuba ya Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango kuhusu hali ya uchumi wa taifa kwa mwaka wa fedha 2018 na mpango wa maendeleo wa taifa wa mwaka wa fedha 2019/2020, jijini Dodoma leo. Picha na Edwin Mjwahuzi

Muktasari:

Serikali ya Tanzania imetaja malengo matano ya ukuaji wa uchumi mwaka 2019/2020 ikiwa ni pamoja na pato halisi la Taifa kufikia asilimia 7.1 mwaka 2019 kutoka asilimia 7.0 mwaka 2018


Dodoma. Kukua kwa pato halisi la Taifa kufikia asilimia 7.1 mwaka 2019 ikilingaishwa na ukuaji wa asilimia 7.0 mwaka 2018 ni kati ya malengo matano ya ukuaji wa uchumi mwaka 2019/2020.

Malengo hayo yameelezwa leo Alhamisi Juni 13, 2019  na Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango  wakati akiwasilisha bungeni jijini Dodoma taarifa ya hali ya uchumi wa Taifa  mwaka 2018 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa mwaka 2019/2020.

Dk Mpango ameyataja malengo mengine kuwa ni kuendelea kudhibiti kasi ya mfumuko wa bei na kuhakikisha kuwa unabaki kwenye wigo wa tarakimu moja kati ya asilimia 3.0 hadi asilimia 4.5.

“Mapato ya kodi kufikia asilimia 13.1 ya pato la Taifa mwaka 2019/2020 kutoka matarajio ya asilimia 12.1 mwaka 2018/2019.”

“Matumizi ya Serikali yanatarajiwa kuwa asilimia 22.7 ya pato la Taifa mwaka 2019/2020 na nakisi ya bajeti (ikijumuisha misaada) kuwa asilimia 2.3 mwaka 2019/2020,” amesema Dk Mpango.