Matangazo maziwa ya kopo, vyakula mbadala kwa watoto marufuku nchi za Sadc

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto nchini, Ummy Mwalimu akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, kuhusu maazimio ya mkutano wa mawaziri wanaosimamia sekta za Afya na Ukimwi wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) uliofanyika jana. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Mawaziri wa sekta ya afya na Ukimwi wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc) wameweka kanuni za pamoja kuzuia uhamasishaji wa matumizi ya maziwa ya kopo kwa watoto wachanga ili kupambana na tatizo la lishe.

Dar es Salaam. Mawaziri wa sekta ya afya na Ukimwi wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (Sadc) wameweka kanuni za pamoja kuzuia uhamasishaji wa matumizi ya maziwa ya kopo kwa watoto wachanga ili kupambana na tatizo la lishe.

Lishe ni moja ya maazimio matano yaliyotolewa leo Ijumaa Novemba 8, 2019 baada ya mawaziri hao kutoka nchi 16 wanachama jumuiya hiyo   kufanya majadiliano kuhusu changamoto za afya.

Mwenyekiti wa baraza hilo ambaye ni Waziri wa Afya wa Tanzania, Ummy Mwalimu ametoa taarifa hiyo huku akisisitiza kuwa mkutano huo pamoja na mambo mengine wameafikiana kuja na azimio hilo kwa ajili ya kulinda afya ya watoto wachanga na wadogo.

“Tumeweka kanuni za pamoja za katazo la uhamasishaji wa matumizi ya maziwa ya kopo na vyakula mbadala kwa watoto wachanga na wadogo na kumlinda mama anayenyonyesha, yaani likizo ya uzazi,” amesema.

Amesema watoto wengi hawanyonyi katika muda unaotakiwa na kuanza kupewa maziwa hayo mapema.

 “Tumeazimia kutumia mfumo wa kikanda kuboresha lishe kwa watoto na mkakati wa kikanda wa kudhibiti uzito uliozidi na kiribatumbo katika jamii,” amesema.

Amesema wameazimia kuwepo kwa matumizi ya kadi alama za lishe kwa nchi za Sadc.