Mawakala wa vyama vinne waapishwa Babati

Msimamizi wa uchaguzi Jimbo la Babati Vijijini Mkoani Manyara, John Nchimbi akiwaapisha mawakala wa vyama vya siasa watakaoshiriki uchaguzi mkuu.Picha na Joseph Lyimo

Muktasari:

Mawakala wa CCM, Chadema, ACT- Wazalendo na NCCR-Mageuzi wanaapishwa kwa ajili ya kutunza siri katika vituo 498 vya kupiga kura kwenye Jimbo la Babati Vijijini.

Babati. Mawakala wa vyama vinne vya siasa  Babati Mkoa wa Manyara, wameapishwa na msimamizi wa uchaguzi wa jimbo hilo, John Nchimbi kwa ajili ya kutunza siri wakati wa kusimamia uchaguzi huo.

Nchimbi amesema leo Jumatano Oktoba 21 kuwa mawakala wanaoapishwa ni wa vyama vya CCM, Chadema, ACT-Wazalendo na NCCR-Mageuzi.

Nchimbi amesema mawakala hao wataapishwa kwenye kanda tano za Bashnet juu ambao wataapishwa shule ya sekondari Bashnet na  Dareda chini wataapishwa shule ya sekondari Dareda.

Amesema mawakala wa Gorowa wataapishwa kwenye Shule ya Sekondari Chief Dodo, Galapo wataapishwa Shule ya Sekondari Galapo na Mbugwe wataapishwa Shule ya Sekondari Joshua.

"Idadi ya mawakala tutaifahamu baada ya kumaliza shughuli hii ila kuna vituo 498 vya kupiga kura kwenye jimbo letu la Babati Vijijini," amesema Nchimbi.

"Wanatakiwa kuapa kiapo cha kutunza siri mbele ya msimamizi wa uchaguzi siku saba kabla ya siku ya uchaguzi," amesema Nchimbi.