Mawaziri wa mazingira nchi za SADC kukutana Arusha

Muktasari:

Mawaziri wa utalii na mazingira wa nchi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) pamoja na wakurugenzi wa utalii na wanyamapori wanatarajia kukutana Arusha kujadili ukuaji wa sekta ya utalii na mazingira katika nchi hizo.

Arusha. Mawaziri wa utalii na mazingira wa nchi wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) pamoja na wakurugenzi wa utalii na wanyamapori wanatarajia kukutana Arusha kujadili ukuaji wa sekta ya utalii na mazingira katika nchi hizo.

Akizungumza  waandishi wa habari leo Jumanne Oktoba 8, 2019 mkuu wa Mkoa wa Arusha,  Mrisho Gambo amesema mkutano huo utafanyika Oktoba 18 hadi 25 mwaka 2019.

Amesema mkutano wa mawaziri utatanguliwa na mkutano wa wakurugenzi wa wanyamapori, mazingira na

utalii na  kufuatiwa  na wa makatibu Wakuu.

"Mkutano huu ni fursa kwa Mkoa wetu na tunashukuru Serikali tunaamini utatoa fursa za kiuchumi kwa wananchi wa Arusha,” amesema Gambo aliyekuwa pamoja na katibu mkuu wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Profesa Adolf Mkenda.

Gambo amesema kati ya washiriki, 200 ni kutoka nje ya nchi na 300 kutoka maeneo mbalimbali  nchini.

Amesema katika kuhakikisha mkutano huo unafanyika katika hali ya amani na ufanisi kila nyanja wameamua kukaa na  wamiliki wa hoteli na vyombo vya usafiri ili wajipange jinsi ya kutoa huduma bora kwa wageni hao.

Kwa upande wake Profesa Mkenda amesema mbali na kuhudhuria mkutano huo wageni hao watapata fursa ya kutembelea hifadhi za wanyama ili waweze kujionea vivutio vya utalii vilivyopo nchini.