VIDEO: Mbatia ataka hospitali binafsi kujitokeza kuwahudumia majeruhi ajali ya lori

Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo, kuhusu ajali ya moto iliyotokea Morogoro juzi. Kushoto ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa wa chama hicho, Honesti Mombuli. Picha na Ericky Boniphace

Muktasari:

Hospitali binafsi zimeombwa kusaidia kuwahudumia majeruhi wa ajali ya lori la mafuta la Morogoro nchini Tanzania iliyotokea Jumamosi iliyopita ya Agosti 10, 2019 na kusababisha vifo na majeruhi.

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa chama cha upinzani nchini Tanzania cha NCCR-Mageuzi James Mbatia ameziomba hospitali binafsi kushiriki katika kuwahudumia majeruhi wa ajali ya lori iliyotokea eneo la Msamvu mkoani Morogoro kwa kuwa wanapitia mateso makubwa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumatatu Agosti 12,2019 jijini Dar es Salaam, Mbatia amesema licha ya kazi kubwa inayofanywa na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) katika kuwahudumia majeruhi hao na Hospitali ya Rufaa Morogoro lakini mazingira ya wodi waliyohifadhiwa si nzuri kwa hali zao.

Amesema chumba walichohifadhiwa majeruhi hao ni kidogo na hakiruhusu kupata hewa ya kutosha, jambo linalowasababishia waendelee kupata maumivu makali.

“Hospitali binafsi zijitokeze hata kila moja kuchukua wagonjwa wawili, wakaweke katika mazingira mazuri yenye viyoyozi itawasaidia hawa kuliko walivyowekwa wote pamoja pale wodini,” amesema Mbatia ambaye pia ni mtaalamu wa majanga

“MNH imefanya kazi kubwa na hata madaktari wanajitahidi sana kuokoa maisha yao, wale watu wana majeraha makubwa tuwasaidie,” amesema

Mbatia ambaye pia ni mbunge wa Vunjo amesema kama hilo litashindikana basi ni vyema ukatengwa ukumbi mkubwa na majeruhi hao wakahudumiwa hapa.

“Jeshi linajua namna ya kukabiliana na majeruhi ya majanga ya aina hii, ni heri wawe kwenye ukumbi mkubwa wenye viyoyozi ili wawe katika mazingira yanayosaidia majeraha yao kupona,” amesema Mbatia

Ajali ambayo anaizungumzia Mbatia ni ile iliyotokea Jumamosi ya Agosti 10, 2019 eneo la Msamvu mkoani Morogoro na kusababisha vifo vya watu 71 na majeruhi 53.

Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi