VIDEO: Mbowe aeleza mwanae alivyougua ugonjwa wa corona

Mwenyekiti wa Chadema na Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chadema na Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe ameeleza kuwa mwanaye aitwaye Dudley ameugua ugonjwa wa corona ambao nchi mbalimbali zinafanya kila juhudi kupambana nao.
Taarifa iliyotolewa na kiongozi huyo wa upinzani bungeni, imeeleza kuwa, ni kweli mwanae Dudley amethibitika kupatikana na virusi vya corona baada ya kupata homa za vipindi, kuumwa kichwa mfululizo na kukohoa kwa siku tano.
“Mama yake, ambaye ni Daktari alipobaini hali hiyo alizitaarifu mamlaka za Serikali zinazoshughulikia janga hili nazo zilimtaka kijana apelekwe Hospitali ya Mwananyamala, Dar es Salaam kwenye vipimo zaidi ambapo ilithibitika rasmi kuwa ana virusi vya corona” ilieleza taarifa ya Mbowe
Mbunge huyo alieleza kuwa timu ya Serikali imeendelea kutoa ushirikiano na ufuatiliaji wa karibu kwa familia yake yote ikiwemo ushauri nasaha kwa wanafamilia na marafiki wengine waliokutana na Dudley katika mikusanyiko mbalimbali ikiwemo kuwaweka wengine karantini.
Mbowe amesema kuwa hali ya mwanaye Dudley sasa imeimarika ambapo homa zimekwisha, kichwa kimepona licha ya kuwa bado anakohoa kiasi na yuko chini ya uangalizi maalum kwenye karantini.