Mchungaji Msigwa, Heche wajisalimisha mahakamani

Muktasari:

  • Baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuamuru wabunge wanne wa Chadema kukamatwa kwa kukiuka masharti ya dhamana, wawili wamejisalimisha mahakamani hapo leo Jumatatu Novemba 18, 2019.

Dar es Salaam. Baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuamuru wabunge wanne wa Chadema kukamatwa kwa kukiuka masharti ya dhamana, wawili wamejisalimisha mahakamani hapo leo Jumatatu Novemba 18, 2019.

Waliojisalimisha ni John Heche (Tarime Vijijini) na Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini). Walikamatwa na polisi baada ya kufika mahakamani hapo.

Ijumaa Novemba 15, 2019 mahakama hiyo iliamuru wabunge hao wawili na wengine, Halima Mdee (Kawe) na Ester Matiko (Bunda) kukamatwa kwa kukiuka masharti ya dhamana.

Amri hiyo ilitolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba baada ya siku hiyo wabunge hao kutokuwepo mahakamani bila taarifa yoyote. Hata wadhamini wao pia hawakuwepo.

Hakimu huyo pia alitoa hati ya wito wa wadhamini wa wabunge hao kujua sababu za kutowapeleka washtakiwa mahakamani.

Mchungaji Msigwa na Heche baada ya kukamatwa leo mahakamani hapo waliunganishwa na Halima aliyefikishwa mahakamani mapema asubuhi akitokea kituo cha polisi Oysterbay.

Ilipofika saa 4: 20 asubuhi, washtakiwa hao watatu walitolewa mahabusu na kuchukuliwa na gari la polisi aina ya Toyota Landcruiser kupelekwa kituo hicho cha polisi.

Wakili wa utetezi, Peter Kibatala amelieleza Mwananchi kuwa washtakiwa watafikishwa mahakamani kesho Jumanne Novemba 19, 2019 katika kesi ya uchochezi inayowakabili pamoja na wenzao watano.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe, naibu makatibu wakuu, Salum Mwalimu (Zanzibar) na John Mnyika (Bara); katibu mkuu wa chama hicho, Dk Vicent Mashinji na mbunge wa Tarime Mjini, Esther Matiko.

Kwa pamoja wanakabiliwa na  mashtaka 13, ikiwemo kula njama, kufanya mkusanyiko wenye ghasia na kuhamasisha hisia za chuki.

Pia, wanadaiwa kushawishi hali ya kutoridhika, uchochezi wa makosa yanayodaiwa kutendeka kati ya Februari 1 na 16, 2018, jijini Dar es Salaam.