Mdee ataka wananchi wanaopisha ujenzi wa barabara walipwe fidia

Muktasari:

  • Wabunge wanawake wa Chadema leo wameingia bungeni wakiwa wamevalia sare za vitenge kama ishara ya kumpokea mbunge mwenzao Halima Mdee ambaye hakuwepo bungeni kwa muda.

Dodoma. Adhabu ya kuwa nje ya Bunge kwa muda haikuweza kumsahaulisha Mbunge wa Kawe (Chadema) Halima Mdee kuhusu madai ya wananchi wanaovunjiwa nyumba zao kupisha ujenzi wa barabara.

Mdee ambaye alikuwa nje ya Bunge tanu Aprili 2019 kutokana na kutumikia adhabu ya kutohudhuria mikutano miwili ya Bunge baada ya kuunga mkono kauli ya aliyekuwa Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Mussa Asad aliyoitoa kuhusu alichokiita 'bunge ni dhaifu.'

Leo Jumatatu Novemba 11, 2019 ameingia bungeni huku wabunge wanawake wa Chadema wakiwa wamevalia sare za vitenge sawa na alichokuwa amevaa.

Dakika tano tangu alipoingia, alipata nafasi ya kuuliza swali la nyongeza na alipopewa nafasi aliuliza kuhusu fidia kwa wananchi wanaopisha ujenzi wa barabara ya Makongo - Goba hadi Chuo cha Ardhi akiomba Wizara kuwalipa fidia wananchi.

"Mheshimiwa Spika, natambua juhudi za serikali katika kupanua barabara Makongo-Goba hadi Chuo cha Ardhi, lakini kuna wananchi ambao wanavunjiwa majengo yao, je nini commitment ya serikali kwa wananchi wale," amehoji Mdee.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe amesema katika malipo ya fidia kinachoangaliwa zaidi ni sheria za nchi siyo kitu kingine.

Ujenzi wa barabara hiyo ulizinduliwa Novemba 1, 2019 na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ambapo utagharimu Sh8.9 bilioni.