Mfungwa aliyeachiwa kwa msamaha wa Magufuli aeleza alichojifunza jela

Wafungwa walioachiliwa kwa msamaha  wa Rais Wakitoka nje ya Gereza la Butimba

Muktasari:

Timotheo Silas aliyehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la unyang’anyi mwaka 2000 ameachiwa huru leo Jumanne Desemba 10, 2019 kwa msamaha wa Rais John Magufuli na kueleza mambo kadhaa aliyojifunza alipokuwa jela.

Mwanza. Timotheo Silas aliyehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la unyang’anyi mwaka 2000 ameachiwa huru leo Jumanne Desemba 10, 2019 kwa msamaha wa Rais John Magufuli na kueleza mambo kadhaa aliyojifunza alipokuwa jela.

Alihukumiwa kifungo Agosti 29, mwaka 2000 akiwa na umri wa miaka 20.

Silas ni kati ya wafungwa 79 waliochiwa huru katika gereza la Butimba mkoani Mwanza.

Jana katika maadhimisho ya miaka 58 ya Uhuru wa Tanganyika, Rais John Magufuli alitangaza msamaha kwa wafungwa 5,533 waliopo magereza mbalimbali nchini.

Akizungumza nje ya gereza hilo Silas amesema, “tunaomba msamaha  kwa viongozi wote wa Tanzania kwa makosa tuliyoikosea jamii. Napenda kumueleza Rais kwamba sisi ni miongoni mwa wafungwa tuliovalishwa nguo za Magereza zilizoandikwa urekebishaji.”

“Kazi ya urekebishaji ina changamoto kubwa ila Magereza wamejitahidi. Mimi nimeingia gerezani nikiwa na miaka 20, nilihukumiwa kifungo Agosti 29, 2000. Sikuwa na taaluma yoyote lakini Magereza walituhimiza na kutufundisha mambo mbalimbali. Gerezani kuna fursa nyingi kama kufundishwa kulima kilimo bora cha mbogamboga.”