Mgombea Chadema kubana wawekezaji wachangie maendeleo

Rungwe. Mgombea ubunge kwa tiketi ya Chadema katika Jimbo la Rungwe, Sophia Mwakagenda amesema akipata ridhaa atahakikisha inakuwepo sheria ya kuwabana wawekezaji wasiochangia miradi ya maendeleo ya wananchi.

Mwakagenda amesema katika mkutano wake wa kampeni wa kuomba kura uliyofanyika katika Kijiji cha Ilundo, Kata ya Kiwira wilayani humo.

"Wananchi natambua matatizo yenu ya miundombinu ya maji, barabara na afya na wakati kuna wawekezaji kibao wa viwanda vya maparachichi, maji na kampuni za ununuzi wa chai, cocoa, ndizi na maziwa wanaopita kwenye barabara za eneo hilo, hivyo atahakikisha wanachangia maendeleo ya halmashauri," alisema.

Kwa upande mwingine Mwakagenda amesema atashughulikia suala la soko la maziwa la ndani na nje ya nchi kwa kuwa wananchi wengi katika Jimbo hilo wanajihusisha na kilimo na ufugaji ili waweze kunufaika na rasilimali hizo wanazozalisha kwa wingi.