Miili 21 yafanyiwa DNA Morogoro, mazishi kufanyika leo

Muktasari:

Serikali ya Tanzania imetoa utaratibu wa awali wa ndugu kutambua miili ya wapendwa wao waliofariki katika mlipuko wa moto uliosababishwa na lori la mafuta ya petroli kuanguka eneo la Msamvu mkoani Morogoro.


Morogoro. Serikali ya Tanzania imefanya utaambuzi wa vina saba (DNA) kwa miili 21 kati ya 64 iliyotokana na ajali ya moto wa lori lililokuwa limebeba mafuta ya petroli kuanguka na kulipuka eneo la Msamvu mkoani Morogoro.

Sanjari na vifo hivyo, watu 70 waliojeruhiwa, 12 kati yao wamehamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Dar es Salaam kwa matibabu zaidi huku wengine wakiendelea na matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Morogoro.

Hayo yalisemwa jana Jumamosi usiku Agosti 10, 2019 na Waziri wa nchi ofisi ya waziri mkuu,Sera, Bunge,Ajira, Kazi,Vijana na Wenye Ulemavu, Jenista Mhagama alipozungumza na wanahabari katika Hospitali ya Rufaa Mkoa wa Morogoro.

Waziri Mhagama alisema kulikuwa na magari ya kubeba wagonjwa ya kutosha ya kuwachukua majeruhi na kuwawahisha Dar es Salaam.

"Utaratibu wa kuhakikisha majeruhi hao wanasafiri salama barabarani na usalama wao umefanyika chini ya wizara ya mambo ya ndani na vikosi vya usalama barabarani kwa uharaka zaidi."

 "Wizara imetengeneza utaratibu wa kutosha chini ya uangalizi mkubwa kwa timu ya madaktari na wauguzi," alisema

Alisema tayari madaktari wasiopungua 10 wameripoti mkoani Morogoro kutoka Hospitali Kuu ya Dodoma ya Benjamin Mkapa na ile ya Muhimbili ili kuongeza nguvu kwa kushirikiana na madaktari wa mkoa wa Morogoro.

Alisema Serikali kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD) imehakikisha imeleta vifaa tiba vyote na dawa kwa ajili ya kuhudumia majeruhi.

Waziri huyo pia alisema wataanza kuruhusu kufanya utaambuzi ndugu wa wagonjwa ambao walishapokelea ambao ndugu 33 wameshajitokeza kutambua hao wagonjwa ambao idadi yao ni 70 na suala hilo la utaambuzi litaendele.

"Kazi ya utaambuzi iitaendelea kwa siku ya Jumapili (leo) na tayari wameanza utaambuzi," alisema.

Alisema katika vifo 64 kati ya hivyo utaambuzi wa vina saba umeanza na itatolewa ruhusa ya kufanya utambuzi wa ndugu wa marehemu kwani miili ya merehemu sio nzuri.

"Lakini tumeonelea kazi ambayo ni muhimu ya kwanza ni kuchukua vina saba vya marehemu wote, ili kama hata marehemu hawatatambuliwa itakuwa ni rahisi kwa Mtanzania yoyote ambaye atakuja na kufikiri kwamba miongoni mwa hao labda anaweza Kuwa na ndugu itakuwa rahisi kwa kumbukumbu itakayokuwepo, hata kama itakuwa ni baada ya kuzikwa,"   alisema Mhagama

Alisema makubalianao kazi ya kuchukua vina saba unafanyika usiku kucha chini ya usimamizi wa mkenia mkuu wa serikali pamoja na polisi na kwamba itatakiwa kukamilika kabla ya saa 12 asubuhi ya leo Jumapili Agosti 11, 2019.

Alisema kazi hiyo itaenda sambamba na miili kuwekewa dawa ili isiharibike haraka na suala la utambuzi wa marehemu itaanza leo Jumapili saa 2 asubuhi ili kuipa nafasi timu iweze kupata nafasi ya kukamilisha uchukuaji wa vina saba.

Hata hivyo, alisema mpaka jana usiku saa 5 walikuwa wamepokea Watanzania 43 wameshajitokeza  ambao wanaohisia kati ya miili hiyo 64 ni ndugu zao.

 Pia alisema wanaotarajiwa suala la mazishi kwa awamu ya kwanza linaweza kuanza saa 10 jioni leo na  itategemea nafasi ya kutosha ya ndugu kutambua miili ya ndugu zao.

"Kama ndugu atataka kwenda kuzika wenyewe ndugu zao hakutakuwa na shida na tutaanza na Ile miili ambayo inaonyeshwa inashindwa kuhimili na kutaka kuharibika," alisema Mhagama

Alisema miili hiyo itazikwa katika makabuli ya Kila Morogoro na kila mmoja atazikwa kwenye kaburi lake na utaratibu wa majeneza umeandaliwa, sanda na kuchimba makabiri yote na kwamba idadi kamili ya makaburi itaendelea kutokana na mahitaji ya ndugu.

Waziri huyo aliwasihi Watanzania kuendelee kuwa wavumilivu huku akiwataka kuendelea kutoa michango yao ili kukamilisha huduma kwa majeruhi.

Aidha alisema chupa za damu salama 166 zimeshapatikana na misaada ya vitu mchanganyiko mbalimbali imepokelewa yenye thamani ya Sh16 milioni.

Alisema gari lililosababisha ajali tayari limeondolewa eneo la tukio na kutakiwa kusafishwa eneo hilo ambapo mkurugenzi wa manispaa ya Morogoro amepewa kazi hiyo ili kuwepo na usalama wa watu.