Mjamzito aliyetaka kujiua ahukumiwa kifungo cha nje

Muktasari:

  • Dementilia Saidia (22) mkazi wa kijiji cha Usagara wilayani Misungwi Mkoa wa Mwanza  amehukumiwa kifungo cha nje cha miezi mitatu baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kutaka kujiua.

Misungwi.  Dementilia Saidia (22) mkazi wa kijiji cha Usagara wilayani Misungwi Mkoa wa Mwanza  amehukumiwa kifungo cha nje cha miezi mitatu baada ya kutiwa hatiani kwa kosa la kutaka kujiua.

Hukumu hiyo imetolewa leo Ijumaa Januari 31, 2020 na Hakimu Mkazi mfawidhi, Eric Marley baada ya mtuhumiwa kusomewa hati ya shtaka lake na kukiri kutaka kujinyonga baada ya kufukuzwa nyumbani, aliyempa ujauzito kumkataa.

"Nilichanganyikiwa baada ya kufukuzwa nyumbani na aliyenipa mimba kuikataa nikaona bora kujinyonga,” amesema Dementilia Saidia.

Mahakama hiyo baada ya kusikiliza maelezo ya mshtakiwa huyo mwenye ujauzito wa miezi mitatu, ilitoa kifungo cha nje cha miezi mitatu, kumtaka katika  kipindi hicho asikutwe na kosa la jinai.

Awali, mwendesha mashtaka, Ramsoney Salehe amesema Januari 28, 2020 katika kijiji cha Usagala,  Dementilia  ambaye alikuwa mfanyakazi wa ndani alijaribu kujinyonga kwa kutumia  kitenge.

Amesema alikifunga kitenge hicho jikoni na alipoanza kuning’inia aliwahiwa na kuokolewa, jambo alilodai ni kinyume na sheria kifungu cha 217 sura ya 16.