Mo Dewji ashika nafasi ya 16 mabilionea Afrika

Dar es Salaam. Mfanyabiashara maarufu nchini Mohammed Dewji (Mo)ametajwa kuwa miongoni mwa mabilionea 20 wa Afrika kwa ripoti ya mwaka 2020 licha ya utajiri wake kupungua kwa Dola milioni 300 (Sh692.67 bilioni).

Katika orodha hiyo ya jarida mashuhuri la Forbes kwa mwaka huu limemtaja Mo mwenye miaka 44 kama bilionea namba 16 huku mfanyabiashara wa saruji, sukari na unga (Aliko Dangote wa Nigeria) akiongoza orodha hiyo.

Utajiri wa Mo umetajwa kufikia Dola bilioni 1.6 (Sh3.69 trilioni) na anayeshikilia namba moja utajiri wake ni Dola bilioni 10.1 (Sh23.31trilioni) naye utajiri wake ukiwa umepungua kutoka bilioni 10.3 (Sh23.78 trilioni) mwaka jana.

Katika orodha ya jarida hilo mwaka jana Mo ambaye ni raia wa Tanzania anayefanya biashara mchanganyiko alikuwa nafasi ya 14 akiwa na utajiri wa Dola bilioni 1.9 (Sh4.3trilioni) hivyo kwa mwaka huu ameshuka nafasi tatu.

“Imepungua Dola milioni 300 (Sh692.67 bilioni), lakini nina watu 32,000 na mwaka huu natarajia kuwekeza Sh500 bilioni hapa hapa nchini na uwekezaji huo utatoa ajira 100,000 kwa Watanzania,” alisema Mo baada ya ripoti hiyo akiwa ndiye Mtanzania pekee aliyeingia katika orodha hiyo.