Mtoto wa mkuu wa majeshi Tanzania afariki ajali ya ndege

Muktasari:

Watu wawili wamekufa katika ajali  ya ndege iliyotokea katika uwanja wa ndege Seronera uliopo katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti nchini Tanzania, akiwemo mtoto wa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi nchini (CDF), Jenerali Venance Mabeyo, Nelson Mabeyo,  

Dar es Salaam. Nelson Mabeyo, mtoto wa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi nchini Tanzania (CDF), Jenerali Venance Mabeyo ni miongoni mwa watu wawili waliofariki katika ajali ya ndege ya Kampuni ya Auric iliyotokea leo asubuhi Jumatatu Septemba 23,  2019.

Nelson ndio  alikuwa rubani wa ndege hiyo iliyoanguka katika uwanja mdogo wa ndege wa Seronera uliopo ndani ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti nchini Tanzania.

Ndege hiyo ilianguka saa 1:30 asubuhi wakati ikipaa katika uwanja huo kwenda mkoani Arusha.

Habari za uhakika kutoka mamlaka ya viwanja wa ndege imeeleza kuwa Nelson aliondoka na ndege hiyo jana katika uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam.

Akizungumza na Mwananchi katika uwanja wa ndege wa Soronera, Msimamizi wa Kampuni ya Auric, Peter Kimaro amesema Nelson amefariki katika ajali hiyo akiwa na Nelson Orutu ambaye ni rubani mwanafunzi.

“Baada ya kuhakiki na kuona ndege iko sawa na kuruhusiwa kuruka kwenda Gurument kuwachukua wageni kuwapeleka KIA (Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro), walipoingia na kuondoka na mimi  nikajua wako sawa,” amesema na kubainisha kuwa Nelson ni mtoto wa mkuu huyo wa majeshi.

Amesema baada ya kuona ndege imeshika mwendo kisha ikapaa kidogo, badala ya kunyooka juu ikakata kona, “na mimi nikashangaa kuona vile kisha ikagonga choo cha uwanjani na kuanguka na wote walifia ndani ya ndege.”

Amesema jeshi la zima moto na uokoaji waliwahi kuzima moto na miili imehifadhiwa katika Zahanati ya Soronera ikisubiri utaratibu mwingine.

Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi