Mwili wa mchekeshaji Martha kuzikwa kesho Dar

Muktasari:

Mwili wa mchekeshaji,  Martha Maiko aliyefariki dunia jana Jumatano Septemba 11, 2019 utazikwa kesho makaburi ya Tabata Kimanga, Dar es Salaam.

Dar es Salaam. Mwili wa mchekeshaji,  Martha Maiko aliyefariki dunia jana Jumatano Septemba 11, 2019 utazikwa kesho makaburi ya Tabata Kimanga, Dar es Salaam.

Akizungumza leo Alhamisi Septemba 12, 2019 mwanzilishi wa jukwaa la ucheshi la Cheka Tu, Conrad Kennedy maarufu Coy amesema mwili wa Martha utawasili nyumbani kwao Kivule Ndombole kwa Mhaya saa 2  asubuhi, utaagwa saa 5 na kuanza safari kuelekea makaburini.

 “Mara ya kwanza nilikutana naye mwaka 2016  akaniambia ni mchekeshaji   angependa kuwa kwenye shoo ya Cheka Tu.”

“Hata hivyo nisiwe muongo kwa kipindi hicho Martha alikuwa hajaiva vizuri kwenye uchekeshaji, ikatulazimu kumuweka benchi kwa mwaka mzima na mwaka 2017 ndio alianza kupanda jukwaani,” amesema Coy.

Amesema Martha alikuwa mfano wa kuigwa kwa uthubutu wake wa kuamini katika kipaji chake licha ya siku za nyuma watu kumponda kuwa hawezi.

 “Tunashukuru ilifika mahali watu wakaanza kumkubali kwa sababu  Cheka Tu pia ni mahali pa kuongeza ujuzi wa wasanii wa vichekesho na ndio maana hata leo watu mbalimbali wanamlilia wakijua wamepoteza kipaji,” amesema.