ANTI BETTIE: Naonekana baharia, tatizo liko kwa jogoo wangu ananiangusha

Habari Anti!

Nina tatizo kimuonekano, ni baharia lakini nikiwa ndani ni zaidi ya mzee wa miaka 60. Nakosa ushirikiano kati ya akili yangu na maumbile yangu ya faragha.

Ninatamani kujamiiana, lakini maumbile yangu hayanipi ushirikiano, yanachelewa kusimama na yakisimama ni dakika moja nimemaliza na hapo tukutane tena wiki ijayo.Nifanyeje?

Pole sana. Hapo ninashindwa kuwa na jibu la moja kwa moja, kwani sifahamu hali hiyo ilianzaje.

Ila wataalamu wa afya wanashauri mambo kadhaa, kama kupunguza unywaji wa pombe, uvutaji sigara, msongo wa mawazo.

Ushauri wangu kwanza wanawake unaokuwa nao umewapenda kutoka moyoni au imetokea tu ukawa nao.

Pia usiende faragha na mwanamke uliyempania sana, hiyo inachangia kukosa kujiamini na mwili kutoafikiana na akili ambayo inataka kujamiiana na wewe haupo tayari.

Jambo la mwisho nakushauri ukaonane na daktari inawezekana pia una tatizo la kiafya ambalo linahitaji ushauri wa kitabibu.

Umri namba kama mnapendana muoe

Mimi ni kijana wa miaka 26, nina mpenzi amenizidi umri. Ana miaka 41, ananipenda kupitiliza na ninaweza kusema hakuna mwanamke aliyewahi kunipenda kama huyu.

Anataka nimuoe je, kwa umri wake naona ni vitu viwili tofauti nifanyeje?

Jiulize kwanza mapenzi ni nini. Jibu utakalopata ndilo litakuwa la msingi. Langu mimi ni kupendana na suala la umri ni namba. Inawezekana una hofu ya kutokuwa na familia, wanawake wanapata watoto hadi miaka 45, hivyo huyo anaweza kukuzalia kabisa na maisha yakaendelea. Nakukumbusha ndoa ni maisha hayaangalii umri, kinachotakiwa muelewane.

Unaweza ukaoa mke kijana au wa umri wako akakusumbua. Hivyo sikiliza nafsi yako kama unampenda na yeye anakupenda muoe, ndoa ni maisha na hayahitaji kujaribu.

Mchumba wangu ni mume wa mtu je, ananipenda kweli?

Nina mchumba wangu, lakini ni mume wa mtu. Je, ana mapenzi ya kweli kangu?

Sijakuelewa kabisa. Labda ungeniambia ni dini gani, tofauti na hapo huwezi kuwa na mchumba ambaye ni mume wa mtu.

Sitaki kuingia ndani kwenye imani nyingine, lakini kama wewe unaamini kwenye Ukristo unaoruhusu mke na mume mmoja, achana na hiyo habari na huyo mwanaume anakupotezea muda hawezi kukuoa. Anakuita mchumba ili umpe anachokitaka akikinai ataondoka, ila kama ni Muislamu, mnaweza kuoana lakini kuna taratibu zake ambazo lazima azifuate kwanza.