Nyumba 300 kubomolewa Tanga, wananchi wamwomba Rais Magufuli awasaidie

Muktasari:

Zaidi ya kaya 900 zinatarajia kukosa mahala pa kuishi kutokana na nyumba walizokuwa wakiishia 300 kubomolewa kupisha upanuzi wa uwanja wa ndege wa Tanga nchini Tanzania.


Tanga. Zaidi ya nyumba 300 zimeanza kubomolewa ili kupisha upanuzi wa uwanja wa ndege wa Tanga nchini Tanzania.

Kutokana na ubomoaji huo zaidi ya kaya 900 zinatarajia kukosa mahala pa kuishi.

Shughuli ya ubomoaji imeanza leo Jumatano Septemba 18, 2019 kwa greda kuonekana likivunja nyumba hizo huku askari wa jeshi la polisi na maofisa kutoka vyombo mbalimbali vya dola wakiwa ni wasimamizi.

MKuu wa Wilaya ya Tanga, Thobias Mwilapwa amesema shughuli hiyo ya ubomoaji wa nyumba hizo inatokana na Serikali kuwa katika mpango wake wa upanuzi wa uwanja huo ili ziweze kutua ndege kubwa wakati wowote.

Wakizungumza wakati ubomoaji ukiendelea wakazi mtaa wa Njombe, Mperani  na Majonjo, Sinza kata ya masiwani mkoani Tanga wamesema wameshangazwa na uamuzi huo kwa sababu wanafahamu Mahakama Kuu imeweka zuio hadi kesi ya msingi itakapoamuliwa.

Ramadhani Chombo ambaye ni Katibu Mwenezi wa Chama cha Mapinduzi CCM wa kata hiyo amesema anajua kesi ipo mahakamani lakini ameshangazwa kuona ubomoaji ukiendelea bila taarifa yoyote kutolewa.

Amemuomba Mwenyekiti wa CCM, Ras John Magufuli kuingilia kati swali hilo ili haki yao iweze kupatikana.

Halima Juma mkazi wa Sinza amesema yeye mpaka sasa hajui pakwenda kwani tayari nyumba yake imevunjwa  na vyombo vyake vipo nje mpaka.

Naye Rehema Jawadu akizungumza huku akitokwa machozi amesema hana mume, anaishi na wadogo zake mpaka sasa anawaza atakwenda wapi na kwamba ni bora wangewapa taarifa ya uwepo wa shughuli hiyo ya kuvunja nyumba ili waweze kujiandaa.