Profesa Kabudi ‘awananga’ wanaokamata ndege za Tanzania

Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Profesa Palamagamba Kabudi

Muktasari:

Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Profesa Palamagamba Kabudi amesema walioshikilia ndege aina ya Bombardier Q400 nchini Canada wameshindwa na hawataweza.

Mwanza. Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania, Profesa Palamagamba Kabudi amesema walioshikilia ndege aina ya Bombardier Q400 nchini Canada wameshindwa na hawataweza.

Profesa Kabudi amesema hayo leo Jumamosi Desemba 14, 2019 katika uwanja wa ndege wa Mwanza kwenye hafla ya kuipokea ndege hiyo.

Novemba 23, 2019 katika hafla ya kuapishwa kwa mabalozi mjini Dodoma,  Waziri Kabudi alieleza kukamatwa kwa ndege hiyo nchini Canada.

Msomi huyo alisema aliyesababisha Bombardier kukamatwa ni Hermanus Steyn, raia wa Afrika Kusini ambaye alifungua kesi ya madai Mahakama Kuu nchini Afrika Kusini akidai fidia ya dola 33 milioni.

Kesi hiyo ilisababisha Mahakama hiyo kuizuia ndege ya Tanzania aina ya  Airbus A220-300 kuondoka nchini humo Agosti, 2019.

Steyn, anadai fidia baada ya mali zake kutaifishwa na Serikali ya Tanzania mwaka 1980. Hata hivyo, Septemba 3, 2019 mahakama hiyo iliamuru ndege hiyo iliyokuwa imezuiwa katika uwanja wa ndege wa Oliver Tambo kuachiwa baada ya Serikali kushinda kesi bila kutoa fedha yoyote.

Akizungumza katika hafla hiyo leo Profesa Kabudi amesema, “leo ni ushahidi tosha wameshindwa, wameshindwaa, wameshindwaa.  Haya anayoyafanya Rais sio kwa faida yake bali ni kwa faida wa nchi yote," amesema Profesa Kabudi.

 

Endelea kufuatilia Mwananchi kujua kinachoendelea