Profesa Mseru: Nyerere ndio muasisi bima afya ya jamii

Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Profesa Lawrence Mseru

Muktasari:

  • Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Profesa Lawrence Mseru amesema mwalimu Julius Nyerere ndio muasisi wa bima ya afya ya jamii mwaka 1962.

Dar es Salaam. Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Profesa Lawrence Mseru amesema mwalimu Julius Nyerere ndio muasisi wa bima ya afya ya jamii mwaka 1962.

Amesema mpaka sasa mwitikio wa mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) na bima ya afya ya jamii (CHF) ni asilimia 33.

Profesa Mseru ameeleza hayo leo Ijumaa Oktoba 11, 2019 wakati akizungumza katika kongamano la siku mbili la  kumbukizi ya Mwalimu Nyerere lililoandaliwa na taasisi ya uongozi kwa ushirikiano na  UDSM.

Amesema japo Serikali wakati huo hakikuwa kubwa kama sasa, lakini Nyerere alijua mahitaji ya wananchi  na changamoto wanazozipata kwa kutokuwa na utaratibu huo.

"Kwa wakati ule mwalimu alimtafuta mtaalamu baada ya kuwasiliana na Serikali ya Israel ili atafiti namna gani bima ya afya kwa wananchi wake itawezekana," amesema Mseru.

Amesema mkurugenzi wa bima ya afya wa Israel wakati huo,  Dk Channan Lachman ndio aliyewasili nchini kufanya utafiti huo.

"Serikali ya mwalimu ilimuhitaji mtaalamu huyu kujua jinsi makundi ya jamii kama waajiri, waajiriwa, familia zao na wananchi waliojiajiri mijini na vijijini wanawezaje kunufaika na bima hiyo," amesema mkurugenzi huyo wa Muhimbili.

Amesema kitendo cha mwalimu kuanza mapema kuhamasisha bima ya afya Watanzania walihitaji kumuelewa zaidi.

Ameeleza kuwa MNH inalipa kati ya Sh500 na Sh600 milioni kwa mwezi kwa wanaoishindwa kulipa gharama za matibabu.

"Hii ni kati ya Sh6 hadi Sh7 bilioni kwa mwaka kwa watu wanaohitaji matibabu lakini hawawezi kujigharamia," amesema.

Profesa Mseru amesema ni vyema jamii iitikie wito wa mwalimu kuwa na bima ya afya.

Mgoda wa Kigoda cha Mwalimu Nyerere cha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam,  Profesa Rwekaza Mukandala amesema  katika mkakati wa kupambana na maadui watatu maradhi, ujinga na umaskini.

"Kwa hiyo tunafanya kongamano kuona yale yaliyoasisiwa na mwalimu yanaendelezwa nchini Tanzania hususani katika kupiga vita umaskini, maradhi na ujinga," amesema Profesa Rwekaza.