RC Gambo azungumzia kugombea ubunge Arusha Mjini

Mkuu wa mkoa wa Arusha (RC) nchini Tanzania, Mrisho Gambo

Muktasari:

Mkuu wa mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo ametumia mkutano wa Jumuiya ya wanawake wa CCM (UWT)  mkoni humo kusema hatogombea ubunge wa Arusha Mjini kama ambavyo imekuwa ikielezwa.

 

Arusha. Mkuu wa mkoa wa Arusha (RC) nchini Tanzania, Mrisho Gambo ameweka hadharani hana nia ya kugombea ubunge wa Arusha kama ambavyo uvumi umekuwa ukisambaa.

Akizungumza katika mkutano wa Jumuiya ya wanawake wa CCM (UWT)  mko Arusha jana usiku Jumatatu Septemba 30,2019, Gambo alisema nafasi ya Mkuu wa mkoa wa Arusha ambayo ameteuliwa na Rais John Magufuli inamtosha.

"Nafasi niliyonayo ni kubwa, wakuu wa wilaya wote wapo chini yangu, wabunge wote wapo chini na taasisi zote za Arusha zipo chini yangu, wabunge wamekuwa wakija kuniomba niwasaidie lakini mimi kama RC naagiza tu," alisema.

Gambo alisema bado anahitaji kuunyoosha mkoa wa Arusha.

Naye Mwenyekiti wa CCM wilaya ya Arusha, Joseph Masawe alisema tangu Mkuu huyo wa mkoa afike Arusha, mji wa Arusha umetulia hakuna vurugu na watendaji wa serikali wanafanya kazi nzuri kutekeleza ilani.

Kwa muda mrefu, Gambo ambaye amekuwa na makazi ya kudumu eneo la kwa Mrombo katika jiji la Arusha amekuwa akitajwa kugombea ubunge wa Arusha hasa kutokana na jitihada zake kuboresha huduma za kijamii katika jiji la Arusha.

Tayari Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema alikwisha kumkaribisha Gambo kwenye kinyang'anyiro cha ubunge katika uchaguzi mkuu ujao 2020 huku akimweleza ajipange vizuri.

Lakini pia Kamanda wa vijana wa CCM mkoa Arusha, Phelemon Mollel ambaye pia amekuwa akitajwa kutaka kuwania tena jimbo hilo mara kadhaa amekuwa akimtaja Gambo huenda atagombea naye ndani ya CCM.