RC Mghwira aeleza njia kupunguza migogoro

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro nchini Tanzania,  Anna Mghwira

Muktasari:

  • Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amesema uwajibikaji, ufanisi na kujitambua ndio njia pekee  ya kupunguza migogoro katika maeneo mbalimbali ya utendaji.

Moshi. Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Anna Mghwira amesema uwajibikaji, ufanisi na kujitambua ndio njia pekee  ya kupunguza migogoro katika maeneo mbalimbali ya utendaji.

Amesema mara nyingi amekuwa akipokea malalamiko mengi ya wateja wa Benki ya NMB benki hiyo kwenye ofisi yake kuhusu huduma wanazozitoa.

Ametoa kauli hiyo leo Oktoba 10, 2019  wakati akikabidhiwa msaada wa vifaa mbalimbali  vya afya na elimu na Benki hiyo vyenye thamani ya sh85 milioni.

"Tukifanikiwa kutoa huduma kwa ufanisi na kwa wakati tutapunguza migogoro mingi ambayo tunaona viongozi wetu wa juu wanapokuja kwenye maeneo yetu wanaishia kusikiliza vitu ambavyo sisi tumeletwa  huku kwa ajili ya kuvitatua ,hii haileti mantiki kabisa.”

"Mameneja mliopo hapa jitahidini kuziba haya mapengo, tujitahidi kuonyesha maono yetu katika huduma hii mliyokabidhiwa,” amesema.

Naye Mkuu wa idara za Serikali wa NMB, Vick Lushum amesema misaada waliyokabidhi leo ambayo ni madawati, meza za maabara, vitanda, magodoro  na mashuka ni kwa ajili ya Halmashauri  za Wilaya ya Hai, Siha, Moshi vijijini, Rombo, Mwanga na Same kwa ajili ya kuboresha sekta ya afya na elimu kwa jamii.