Rais Magufuli agawa vitambulisho vya wamachinga

Muktasari:

  • Rais Magufuli amegawa  vitambulisho 675,000 kwa ajili ya kuwatambua wafanyabiashara wadogo nchini Tanzania, asisitiza ukusanyaji kodi

Dar es Salaam. Rais John Magufuli ametoa vitambulisho 670,000 kuwatambua wafanyabiashara wadogo nchini Tanzania kuhakikisha wanafanya shughuli zao bila kusumbuliwa.
Rais ametoa vitambulisho hivyo leo Jumatatu Desemba 10, 2018 kwenye mkutano wake na watendaji wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), wakuu wa mikoa yote nchini humo kujadili namna ya kuboresha mazingira ya ukusanyaji mapato.
Amesema kwa muda mrefu amekuwa akiiagiza TRA pamoja na halmashauri kutowatoza kodi wajasiriamali wadogo ambao mitaji yao haizidi Sh4 milioni lakini utekelezaji wake umekuwa wa kusuasua.
Kila Mkoa utapewa vitambulisho 25,000 na kila mjasiriamali mdogo atalipia Sh20,000 na fedha hiyo kupelekwa TRA.
Kwa malipo hayo, kila mkuu wa Mkoa atakusanya Sh500 milioni na ikilazimu aagize vitambulisho vingine kwa ajili ya watakaovihitaji.
Rais Magufuli amesema hajaridhishwa na utaratibu wa kuunganisha kitambulisho cha TRA na kile cha Taifa kuwatambua wafanyabiashara wadogo akibainisha baadhi yao kutozwa kodi nje ya maagizo.
 “Suala la kuwasajili wafanyabiashara wadogo linaenda polepole sana, tangu nimetoa maagizo kwamba mamalishe na wamachinga wasisumbuliwe. Unakuta mtu ana mtaji usiozidi Sh4 milioni lakini wanasumbuliwa kila siku anatafutwa kulipa kodi na ushuru wa kila aina,” amesema.
Amesema vitambulisho hivyo ni kwa ajili ya kuanzia na endapo kutakuwa na mahitaji zaidi vitatengenezwa kulingana na mahitaji ya mkoa husika.
“Nimeamua kufanya tofauti, nimechapisha vitambulisho mimi mwenyewe. Mfanyabiashara akishavaa kitambulisho hiki asisumbuliwe na mtu yoyote na kwa vile nimekitoa mimi, sioni mtu atakayeenda kumsumbua,” amesema Rais Magufuli.
Katika hatua nyingine, Rais Magufuli ameeleza kutoridhishwa na kiwango cha ukusanyaji wa mapato nchini Thumo huku akitaja baadhi ya sababu zinazochangia kuwa ni viwango vikubwa vya kodi vinavyotozwa na TRA.
Ameitaka TRA pamoja na Wizara ya Fedha na Mipango kuboresha mazingira ya ukusanyaji mapato ikiwamo kodi ya majengo ili ilingane na hali halisi ya maisha ya Watanzania.