Rekodi kibao Liverpool v Arsenal Jumamosi

Muktasari:

Mabingwa hao wa Ulaya wanapewa nafasi kubwa ya kuendeleza ubabe mbele ya Arsenal kwenye Uwanja wa Anfield.


Kutakuwa hakuna timu ambayo haijapoteza poin ti zozote Jumamosi jioni iwapo vigogo wawili wa Ligi Kuu ya soka ya England, Liverpool na Arsenal watatoka sare kwenye uwanja wa Anfield.

Lakini Ligi Kuu itabakia na timu moja pekee ambayo haijapoteza mchezo iwapo moja ya vigogo hao atakubali kichapo baada ya mabingwa wa soka barani Ulaya, Liverpool kushinda mechi zake za kwanza dhidi ya Norwich City na Southampton, wakati Arsenal ilishinda dhidi ya Burnley na Newcastle.

Timu hizo zilikuwa na mikakati tofauti wakati wa kipindi cha usajili lakini Liverpool ilijikuta zaidi katika kikosi kilichotwaa ubingwa wa Ulaya huku Arsenal ikimwaga fedha kuwanunua Nicolas Pepe, Kieran Tierney na David Luiz.

Arsenal itatakiwa ifanye kazi ya ziada kama inataka kuepukana na wimbi la matokeo mabaya kwenye Uwanja wa Anfield baada ya kuboronga katika mechi sita, Imeshapoteza mechi 13 kwenye uwanja huo, ukiwa ni wa pili kwa Arsenal kupoteza mechi nyingi baada ya Old Traford, uwanja wa Manchester United.

Latika mechi hizo za Ligi Kuu, Arsenal iliruhusu angalau mabao mawili katika kila mechi.

Na Liverpool haina utamaduni huo wa kupoteza poionti kwenye uwanja wake wa nyumbani na rekodi zinaonyesha haijashindwa katika mechi 41. Ni Chelsea tu iliyocheza mechi 86 bila ya kushindwa hadi Oktoba 2008, ndiyo pekee inayowezas kupiku rekodi hiyo ya Liverpool.

Pamoja na hayo, Liverpool imekuwa mbabe dhidi ya timu zinazoshika nafasi sita za juu na timu hizo hazijaweza kuishinda katika mechi 18, huku vigogo hao wakishinda mechi 10.

Ushindi wa mabao 5-1 wa msimu uliopita ambao Liverpool iliupata dhidi ya Arsenal ni kumbukizi tosha ya jinsi mambo yanavyoweza kuwa mabaya kwa Arsenal.

Wachezaji mashoto nyota

Mechi ya Jumamosi pia itakutanisha wachezaji nyota wanaotumia mguu wa kushoto. Mohamed Salah alifunga bao katika mechi ambayo Arsenal ilisambaratishwa na atakuwa amepania kung'ara tena wakati Pepe atakuwa akijaribu kufikia makali ya mchezaji huyo wa Misri baada ya uhamisho ulioweka rekodi Arsenal.

Takwimu za Pepe katika msimu ulioisha akiwa na Lille nchini Ufaransa pia ni nzuri sawa na Salah alivyofanya wakati akiwa Roma kiasi cha kumfanya anunuliwe naLiverpool.

Salah alifunga mabao 15 na kutoa pasi 11 za mabao. Pepe, naye, alifunga mabao 22 na kutoa pasi 11 za mwisho huku akihusishwa katika mabao 33 yaliyotokea katika kila dakika 100.8.

Pia staili za wawili hao zinaweza kulinganishwa, lakini bado Pepe alijaribu kukimbia na mpira mara nyingi (mara 213 dhidi ya 70) na kuchezewa rafu mara nyingi (mara 108 dhidi ya 26) zaidi ya Salah, ambaye anajulikana kwenye Ligi Kuu kutokana na uwezo wake mkubwa wa kukaa na mpira.

Arsenal watakuwa wakitarajia Pepe atawesza kuhamishia makali yake kwenye soka la Uingereza na kupata mafanikio.

Lakini rekodi ya Liverpool nyumbani inaweza kumpa hofu Pepe na Arsenal yake, lakini kiwango cha vigogo hao hakiishii nyumbani Anfield. Liverpool imeshinda mfululizo mechi 11 na ushindi katika mechi ya Jumamosi utawafanya wawe wameshinda mechi 12 mfululizo na kufikia rekodi yao ya ushindi mfululizo.

Kazi ya Arsenal itakuwa ni kumzuia Juergen Klopp na vijana wake kupata matokeo wanayotaka.

Mara ya mwisho Liverpool kupoteza pointi katika Ligi Kuu ilikuwa wakati ilipotoka sare na Everton mwezi Machi. Sare kama hiyo dhidi ya wapinzani wao, Manchester United wiki moja kabla ya Everton ndiyo iliyokuwa mechi nyingine kwa vigogo hao kuipoteza pointi katika mechi 32 ambazo hawakuweza kuziona nyavu.

Arsenal - ambayo imeshinda mechi tatu za Ligi Kuu kujumlisha na ya mwisho ya msimu uliopita - haijaweza kushinda mechi nne mfululizo kwa karibu mwaka mzima, wakati ushindiu utaifanya ishinde kwa mara ya kwanza mechi tatu mfululizo za mwanzoni mwa msimu wa ligi tangu mwaka 2004-05, walipokuwa mabingwa watetezi kwa mara ya mwisho.

Moto upande wa pili

Matarajio mengine katika mechi ya leo ni mabao kwa kuwa mchezo baina ya vigogo hao wawili umeshazaa mabao 155, ikiwa ni idadi kubwa kuliko mechi za timu nyingine za Ligi Kuu.

Wakati Salah ni tishio, Roberto Firmino anategemea kuwa moto tena kwa kuwa ameshafunga mabao saba katika mechi dhidi ya Arsenal kwenye uwanja wa Anfield.

Lakini mashabiki watatetegemea pia kuona moto ukiwaka upande wa pili ambako Pierre-Emerick Aubameyang ameshafunga mabao matatu katika michezo 13 dhidi ya timu sita zinazoshika nafasi ya juu, ikilinganishwa na mabao 31 katika mechi 38 dhidi ya timu nyingine kwenye ligi.

Liverpool ndiyo inayopewa nafasi kubwa ya kushinda ikiwa haijashindwa na Arsenal katika mechi nane na hadi sasa kocha Klopp hajawahi kupoteza mchezo mbele ya Arsenal.