Romy Jones azua maswali idadi ya watoto wa Diamond

Muktasari:

Romy Jones, binamu wa mwanamuziki Diamond Platnumz  amezua maswali mtandaoni baada ya kusema ndugu yake huyo ana watoto watano badala ya wanne wanaotambulika na maelfu ya mashabiki zake jambo ambalo limezua gumzo katika mitandao ya kijamii. Ametoa kauli hiyo baada ya mpenzi wa mwanamuziki huyo, Tanasha Donna kujifungua mtoto wa kiume jana Jumatano Oktoba 2, 2019.


Dar es Salaam. Romy Jones, binamu wa mwanamuziki  Naseeb Abdul maarufu Diamond Platnumz amezua gumzo katika mitandao ya kijamii baada ya kumpongeza ndugu yake ya kupata mtoto wa tano.

Gumzo hilo limetokana na mashabiki wengi wa mwanamuziki huyo kudai kuwa ana watoto wanne na si watano kama alivyoeleza Jones.

Jones ameandika jambo katika ukurasa wa mtandao wa kijamii wa Instagram akimpongeza Diamond baada ya jana Jumatano Oktoba 2, 2019 mpenzi wa mwanamuziki huyo, Tanasha Donna kujifungua mtoto wa kiume.

Diamond anayemiliki tuzo zaidi ya 35 alifurahia kuzaliwa kwa mwanaye huyo  wakati akisherehekea siku yake ya kuzaliwa.

Wakati Diamond  akipongezwa kwa kuwa na watoto wanne, Jones amesema ndugu yake ni baba wa watoto watano.

“Hongera sana kwa kupata mtoto wa kiume kwenye siku yako ya kuzaliwa! Hakika huyo ndio atakua pacha wako, Allah akutunzie, akulindie na akukuzie pia Inshaallah panapo maajaliwa na mimi nitapata japo mmoja wa kukuita  wewe baba.”

“Maana mpaka sasa hivi mimi naitwa baba mkubwa wa watoto watano,” amesema Jones huku baadhi ya maoni ya mashabiki zake wakihoji kuhusu mtoto wa tano.

Zulfa Mohammed aliandika, “Hivi ni watano kumbe.” Huku Jenifer akisema, “kuna mtu anaweza kunisaidia kunielewesha hao watano huyo mmoja sijawahi kumsikia, kumbe alikuwa na watoto wanne?”

Kupitia ukurasa wake katika mtandao wa Twitter, Diamond ameandika “07:28  mchana wa Oktoba 2, 2019 kisha akaweka alama mbili za kopa na katikati au rozi jekundu.”

Mashabiki wa nyota huyo wametoa pongezi zao kupitia mtandao wa Instagram ikiwemo ukurasa rasmi wa redio ya Wasafi (WasafiFm) ambayo Diamond ni mkurugenzi wake.

“@DiamondPlatnumz na @Tanashadonna wamefanikiwa kupata mtoto wa kiume siku ya leo…Huyu ni Mtoto wa kwanza wa Tanasha na wa nne kwa upande wa Diamond, andika chochote kuwapongeza @Diamondolplatnumz na @Tanashadonna kwa kupata Mtoto,” ujumbe ulisomeka hivyo.

Dada wa Diamond Esma ameandika, “Ooops hongereni kwa Baby Boy ila na hongera na mimi najipongeza Aunty sio kwa zoezi lile mwanangu umenikomesha sio kwa kunifanya niwe macho mpaka sasa hivi.”