VIDEO: Sababu za Spika kuzuia hotuba ya upinzani bungeni

Muktasari:

Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amezuia kusomwa kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni kuhusu hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kwa sababu imekiuka kanuni za uendeshaji wa Bunge.

Dodoma. Spika wa Bunge la Tanzania, Job Ndugai amezuia kusomwa kwa maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani bungeni kuhusu hotuba ya bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2020/2021 kwa sababu wamekiuka kanuni za Bunge.


Hotuba hiyo ilikuwa isomwe leo Jumatano Aprili Mosi 2020 na Mbunge wa Kawe (Chadema), Halima Mdee kwa niaba ya Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Bungeni, Freeman Mbowe.
Akizungumza kabla ya Halima kuruhusiwa kuisoma, Ndugai amesema baadhi ya mambo yaliyoandikwa katika hotuba hiyo ni ya uzushi.


Amesema taarifa kuwa aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu kwamba analidai Bunge ni za uzushi na kwamba hakuna mbunge anayedai.
Ndugai amesema ndani ya hotuba hiyo kuna madai kuwa Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani hapati huduma.


Amesema kuwa Mbowe analo gari na kwamba kama kuna tatizo, kama ubovu ni jambo la kuwasiliana na Katibu wa Bunge.


Amesema Mbowe anayo nyumba ambayo aliikataa na badala yake alimpatia mnadhimu wa kambi rasmi ya Bunge (aliyekuwa Lissu) na yeye kuishi kwenye nyumba yake binafsi.
Hata hivyo, amesema Bunge halitoi nyumba kwa mnadhimu wa kambi ya upinzani.


Ndugai amesema ingawa Mbowe alikataa nyumba hiyo lakini amekuwa akipata huduma zote anazostahili kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani ikiwemo ulinzi, mhudumu, maji na nyingine anazostahili.
“Anasema hajapewa wasaidizi lakini tuliwaondoa wasaidizi wote hata wa CCM tuliwakataa kwa sababu ya usalama,” amesema.


Amesema ofisini ana wasaidizi wanne ambao ni katibu muktasi, mhudumu, ofisa mwandamizi na dereva.


Amesema awali alikuwa akiwaruhusu kusoma bajeti kwa kuondoa baadhi ya maeneo lakini hivi sasa hataruhusu kusomwa tena hotuba za namna hiyo.