Serikali ya Tanzania yataja sifa kuajiri watumishi ATCL

Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Atashasta Nditie akijibu swali bungeni jijini Dodoma leo. Picha na Anthony Siame

Muktasari:

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Atashasta Nditiye amesema Serikali ya Tanzania haitumii kigezo cha mvuto kuajiri watumishi wa Shirika la Ndege nchini (ATCL).

Dodoma. Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Atashasta Nditiye amesema Serikali ya Tanzania haitumii kigezo cha mvuto kuajiri watumishi wa Shirika la Ndege nchini (ATCL).

Nditiye ametoa kauli hiyo siku moja baada ya mbunge wa Kigoma Kusini (CCM), Husna Mwilima kusema wahudumu wa ndege za ATCL hawana mvuto kwa wateja.

Kabla ya kuanza kujibu maswali ya wabunge bungeni mjini Dodoma leo Ijumaa Novemba 8, 2019, Nditiye amesema shirika hilo limeanisha sifa mbalimbali za kuajiri ikiwemo mhusika kuwa Mtanzania mwenye umri kuanzia miaka 18 na kuendelea.

Amesema anapaswa kufahamu kwa ufasaha Kiingereza na Kiswahili, kuwa na cheti cha kuongoza ndege au  kufanya kazi katika ndege.

“Sifa ya muhimu ni lazima awe na leseni ambayo inatolewa na Mamlaka ya Anga (TCAA),”amesema.

Ametaja sifa nyingine za ziada ni kuwa na ufahamu wa mambo mbalimbali ya kitaifa, kidunia na utalii.

Amesema pia anatakiwa kuwa na hekima, heshima, maadili na watamchunguza kama anafaa kuajiriwa.

“Sifa nyingine zote zinazozungumzwa sio sifa zinazozingatiwa na ATCL wala Serikali yetu,” amesema Nditiye.