Serikali ya Tanzania yazungumzia ujenzi viwanda 100 kila Mkoa

Muktasari:

Serikali ya Tanzania imesema tangu kuanza kwa mkakati wa ujenzi wa viwanda 100 kila Mkoa, hadi sasa vimejengwa viwanda vipya 3,000

Dodoma. Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Mwita Waitara amesema Tanzania kuna viwanda vipya 3,000 tangu kuanza kwa mkakati wa kujenga viwanda 100 kila Mkoa.

Waitara ametoa kauli hiyo leo Jumatano Juni 12, 2019 bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la nyongeza la  mbunge wa Viti maalum (Chadema), Sophia Mwakagenda aliyetaka kujua ni viwanda vingapi vimejengwa tangu kuelezwa mkakati wa ujenzi wa viwanda 100 kila Mkoa, akidai kuwa mkakati huo ni wa kisiasa.

“Tumeshatenga maeneo mbalimbali katika wilaya ya mikoa na mpaka sasa kuna viwanda vipya 3,000. Huu si mkakati wa kisiasa,” amesema Waitara.

Katika swali lake la msingi Mwakagenda alitaka kujua ni  waraka gani wa Serikali ulioainisha Tamisemi kujenga viwanda 100 ili kuwapa wananchi rejea ya pamoja na kitaifa

Akijibu swali hilo Waitara amesema, “mkakati huu ni sehemu ya mikakati mbalimbali inayotekelezwa na Serikali ya Awamu ya Tano kujenga uchumi wa viwanda uliofungamanishwa na maendeleo ya watu. Tamisemi imeandaa mwongozo wa kubainisha majukumu ya mikoa na mamlaka za serikali za mitaa katika utekelezaji wa sera ya viwanda. Mkakati huo haupaswi kutenganishwa na mipango mingine ya Serikali inayohamasisha ujenzi wa viwanda nchini.”