VIDEO: Serikali yawarejesha watoto wa bilionea Msuya kwenye nyumba ya baba yao

Muktasari:

Mkuu wa wilaya ya Arumeru, Jerry Muro amekutana na wazazi wa bilionea Msuya, watoto wake na baadhi ya wanafamilia upande wa mke wa Msuya ambaye yupo Gereza la Segerea jijini Dar es Salaam na akuagiza watoto wa bilionea huyo kurejeshwa katika nyumbani ya baba yao.


Arusha. Mgogoro wa mali za bilionea Erasto Msuya umechukua sura mpya baada ya leo Alhamisi Oktoba 17, 2019, Serikali ya Tanzania kuagiza watoto kurejeshwa kwenye makazi ya baba na mama yao  ambayo yalikuwa yamefungwa.

Agizo hilo la awali limetolewa na mkuu wa wilaya ya Arumeru, Jerry Muro baada ya kukutana na wazazi wa Bilionea Msuya, watoto wake na baadhi ya wanafamilia upande wa mke wa Msuya ambaye yupo Gereza la Segerea jijini Dar es Salaam akikabiliwa na kesi ya mauaji.

Mke wa bilionea huyo, anatuhumiwa kwa mauaji ya Aneth Msuya ambaye ni dada wa bilionea Msuya.

Wakizungumza baada ya uamuzi huo, mtoto wa bilionea huyo, Kelvin Msuya na babu yake, Elisaria Msuya walikubaliana na uamuzi huo wa awali.

Kelvin (22) anasema anataka yeye na wadogo zake wapewe haki ya kusimamia mali za baba na mama yao na si mtu mwingine.

Anasema  familia ya baba yao inataka kuwanyang’anya mali kwani baada ya mama yao kukamatwa wamefungua kesi upya za kudai usimamizi wa mirathi  ingawa tayari mama yao aliteuliwa wa lengo lao wachukue mali.

 

"Mwanzo babu na shangazi Ester walifungua kesi ikafutwa, Ndeshukuro Sikawa na babu wakafungua ikafutwa sasa amefungua tena bibi peke yake," amesema

 

Anasema ndugu hao walifungula kesi na kutaka kumuunganisha na mama yake lakini alisaidiwa na ndugu wa mama yake na maofisa wa juu wa polisi

 

Hata hivyo, baba wa bilionea huyo, anasema walifunga nyumba za bilionea huyo kutokana na kuzuia upotevu wa mali hasa baada ya kuanza kuibiwa.

 

Alisisitiza baadhi ya mali za bilionea huyo yeye na mkewe walikuwa na hisa ikiwepo mgodi wa Tanzanite ambao alidai ni mali yake, hoteli ya SG na mashamba.

 

Bilionea Msuya aliuawa kwa kupigwa risasi Agosti 7 mwaka 2013 na ameacha nyumba za kifahari zaidi ya tano, magari, hoteli mbili za kitalii, viwanja na mgodi wa Tanzanite.